WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Monday, October 30, 2017

NI HISTORIA MIAKA MIWILI YA JPM NA ELIMU

Na MWANDISHI WETU

NI historia na msimamo mkali. Ndivyo unaweza kusema hasa baada ya Rais Dk. John Magufuli kuisimamia kwa vitendo sera ya elimu bure kwa shule za msingi na sekondari nchini.

Kutokana na hali hiyo, wadau mbalimbali wa ndani zikiwamo taasisi za umma na sekta binafsi zilitangaza kumuunga mkono, huku Serikali ya Uingereza ikivutiwa na mpango huo.
Hatua hiyo inatajwa kama njia ya mafanikio kwa Rais Dk. Magufuli ambaye Novemba 5, mwaka huu anatimiza miaka miwili madarani, huku akitajwa kama shujaa aliyedhamiria kuinua elimu kwa vitendo.

Kitendo cha Rais kutamka hadharani kuwa serikali yake anayoiongoza haitawalipisha ada, gharama za mitihani na michango mingineyo iliyokuwa inawakwaza wazazi na walezi wa wanafunzi  hasa wanyonge na masikini kwa kueleza kutengwa kwa zaidi ya shilingi bilioni 18.7 kila mwezi kwa ajili ya kugharamia mfumo na sera ya elimu bure hapa nchini.

Kadharika, kuasisiwa huko kwa utaratibu huu wa elimu bure kumesababisha kuwepo kwa mafanikio makubwa katika usajili na uandikishwaji wa wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza baada ya kuongezeka kwa idadi kubwa ya wanafunzi waliofikisha umri wa kwenda shule na kujiunga katika mikoa mbalimbali ya sehemu kubwa ya nchi

‘’kwetu sisi hakika tumevuka malengo na matarajio, wakati rais anatuagiza kutekeleza mfumo huu wa elimu bure hatukutarajia kama muitikio ungekuwa mkubwa kiasi hiki…kwa kweli mfumo huu wa elimu bure umesababisha watu wengi zaidi wawaandikishe watoto shule na hivyo kuondoa uwezekano wa kuendelea kuwepo kwa watoto wasiojua kusoma na kuandika katika siku zijazo’’. Alinukuliwa Mtela Mwampamba, Katibu tawala wa wilaya ya Kisarawe.

Aidha akizungumza na gazeti hili mkazi wa Morogoro kihonda Aziza Matiga Malinda amempongeza Rais kwa msimamo wake wa kutoa elimu bure kwa kuzingatia ukweli kwamba unasaidia kuondoa matabaka baina ya watanzania na watu wote wenye sifa za kwenda shule sasa watakuwa wanakwenda shule bila kikwazo wala kizingiti cha ada akitolea mfano yeye anavyoweza kuwasimamia watoto wake watatu kwenda sekondari huku yeye gharama zake zikiwa ni utekelezaji wa majukumu mengine kama mzazi na si ada wala michango ya shuleni.

‘’Unaona mimi ninasomesha watoto watatu hapo, mmoja kidato cha pili na mwingine cha tatu na mmoja darasa la sita, sasa kwa hali yangu hii ningeweza kweli kuwalipia ada na michango mingine hawa watoto wote?..kwa kweli namshukuru sana Mungu kwa kutuletea Rais huyu mwenye Huruma’’. Alisema Aziza

Madawati

Katika kile kinachoonekana kufanikiwa kwa elimu bure kwa kipindi cha miaka miwili ya uongozi wa Rais Dk. John Magufuli, wakuu wa mikoa na wilaya wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutimiza agizo la mkuu huyo wa nchi la kukabiliana na upungufu wa madawati katika shule za msingi na sekondari ili kuhakikisha wanafunzi wanasomea katika mazingira bora.

Mapema mwaka jana, Rais Magufuli aliteua wakuu wapya wa mikoa na baada ya kuapishwa aliwaambia vigezo atakavyotumia kuwapima ni pamoja na kushughulikia tatizo la upungufu wa madawati katika shule za msingi na sekondari ili kuimarisha mazingira ya shule na kufanikisha sera ya kutoa elimu bure kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha nne.

Rais aliwataka wakuu wa mikoa kuhakikisha kuwa hadi kufikia Juni 30, mwaka jana wawe wamelimaliza tatizo la madawati katika shule zote.

Kwa mujibu wa hotuba ya Waziri Mkuu wakati wa kuahirisha Bunge la 11, takwimu zinaonesha hadi kufikia Juni 17, mwaka jana, tayari kulikuwa na madawati mapya 552,630 ambayo yamepatikana kwa njia ya michango mbalimbali na hivyo kufanya shule za msingi kuwa na madawati 2,632,392 sawa na asilimia 77 ya mahitaji na sekondari zikifikisha madawati 1,395,138 sawa na asilimia 93.

Takwimu hizo zinaonesha kuwa katika shule za msingi bado yanahitajika madawati 792,949 sawa na asilimia 23 na sekondari madawati 112,785 sawa na asilimia saba. Taarifa ya Waziri Mkuu inasema kuwa halmashauri 25 kutoka mikoa 13 zimeripotiwa rasmi kukamilisha mahitaji ya madawati ya shule za msingi na halmashauri 46 kutoka mikoa 19 zimekamilisha madawati kwa shule za sekondari.

Katika hotuba hiyo ya kuahirisha Bunge iliyotolewa siku 13 kabla ya Juni 30, mwaka jana, ni wazi kuwa mikoa mingine imefanikiwa kukamilisha mradi huo kabla ya tarehe iliyopangwa na rais.

Hadi ilipofika Juni 30, mwaka jana, mikoa mbalimbali iliripoti kukamilisha mradi wa madawati kwa shule za msingi na sekondari, ambapo Jiji la Arusha likiwa limepitiliza lengo kwa kuwa na madawati ya ziada 180.

Hatua hiyo iliungwa mkono na wadau mbalimbali zikiwamo taasisi za umma, mashirika na sekta binafsi kwa kuunga mkono juhudi za Rais Magufuli kwa kutekeleza sera ya elimu bure kwa vitendo.

Mbali na hilo, pia Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini naye aliunga mkono kazi hizo kwa kutoa madawati 10,000 ambayo alimkabidhi Rais Dk. John Magufuli kama mkakati wake wa kuinua elimu nchini.

Uchunguzi uliofanywa na Jamvi la Habari umeonyesha kwamba hadi kufikia mwezi wa tisa mwaka huu, lengo la upatikanaji wa madawati kwa shule zote hapa nchini lilikuwa limetimia kwa wastani wa asilimia 92.5.

Maabara

Uhamasishwaji wa ujenzi wa Maabara za sayansi shuleni ulioonekana kupokelewa kwa mikono miwili na kuanza kutekelezwa kwa kuwahusisha wananchi, serikali, halimashauri na wadau wa maendeleo unaonyesha kuchagiza uimara wa mfumo wa elimu nchini na kuzidi kummwagia sifa Rais Magufuli.

Tangu ameingia madarakani, Rais amekuwa akiwaagiza wasaidizi wake hasa wakuu wa mikoa na wilaya kuhakikisha kuwa ujenzi wa shule unaenda sambamba na uwepo na maabara za sayansi kwa ajili ya wananfunzi kujifunzia na madawati ili kufikia lengo la Tanzania ya viwanda.

Elimu ya Ufundi
Idara nyingine katika mfumo wa elimu inayopigiwa mstari wa mfano ni uimarishaji wa elimu za ufundi katika maeneo mbalimbali hapa nchini kwa kipindi cha miaka miwili ya uongozi wake.

Katika hotuba na nukuu mbalimbali za kielemu ambazo anazitoa waziri wa elimu na watendaji wa wizara hiyo, ni pamoja  na uchagizwaji na uboreshaji wa vyuo vya ufundi kama vile Veta ambavyo kwa mujibu wa sera na mipango ya serikali ni kwamba inahitajika kuwepo angalau chuo kimoja cha ufundi katika kila wilaya, jambo ambalo limeonyesha kufanikiwa kwa kasi baada ya maeneo mengi nchini kuendelea kujenga vyuo hivyo au kubadili matumizi ya baadhi ya shule ama taasisi au majengo na kuyageuza kuwa vyuo vya elimu za ufundi.

Elimu ya Juu
Pamoja na maboresho mbalimbali yanayoonekana kufanyika katika mfumo wa elimu hasa elimu ya msingi na sekondari,
Kadharika serikali ya awamu ya tano imeonyesha kuwepo kwa mapinduzi makubwa baada ya Rais kuendelea kufanya mambo kadhaa kwa moyo na upendo wa dhati.

Ujenzi wa mabweni mapya ya wanafunzi wa Chuo kikuu cha Dar es salaam katika eneo la barabara ya Sam Nujoma, kurudisha mfumo wa udahili wa wanafunzi ambapo sasa mwanafunzi anaomba moja kwa moja katika chuo husika tena kwa kulipa shilingi elfu kumi tu tofauti na hapo nyuma na kuimarishwa kwa upatikanaji wa mikopo kwa wananfunzi wanaostahili tena kwa wakati kumefanya wanafunzi wengi kumpongeza Rais Magufuli na kumtaka aendelee na moyo huo huo na kwamba wao wataendelea kumuombea kwa Mungu.

‘’mimi nimeanza chuo mwaka jana hapa Udom, kwa kweli sijawahi kupata tatizo lolote hasa kuhusiana na upatikanaji wa mkopo japo mimi nilidahiliwa na TCU, ila napongeza zaidi mfumo wa udahili wa sasa’’. Anasema Hanssy Kibiki mwanafunzi wa chuo kikuu cha Dodoma

Kadharika, akiongea na gazeti hili Johnson Maliyamungu ambaye ni mwanafunzi mteule wa chuo kikuu cha Dar es salaam kampasi ya Mlimani akisomea masuala ya uchumi na biashara anasema ‘’ unajua huko sekondari tulikuwa tunajiandaa kujan chuo kikuu hasa hapa mlimani kugoma…akili zetu zilijiandaa kisaikolojia kwamba huko chuoni tusipotimiziwa mahitaji yetu ni mgomo tu, lakini kwa hii spidi ya serikali yetu wala hatuna sababu ya kugoma tena, Mabweni yamejengwa, mikopo tunapatiwa kwa wakati na juzi tu hapa Rais kasema ameshatoa bilioni 147 kwa ajili yetu, sasa yanini tugome?’’. Alinukuliwa Malyamungu

Mimba shuleni
Katika kuonyesha kuwa hana utani na elimu kwa wananchi anaowaongoza na kwamba anataka watanzania wote wanaostahili kusoma wasome bila kujihusisha na vitendo visivyo vya kiuwanafunzi,
akiwa katika ziara yake mkoani Pwani hivi karibuni, Rais Magufuli alitoa msimamo mkali kuhusu wanafunzi wanaopata mimba wakiwa shuleni na kusema katika muda wote atakaokuwa madarakani, hakuna mwanafunzi wa shule ya msingi na sekondari atakayepata ujauzito atakayeruhusiwa kuendelea na masomo katika shule za umma. 

Akisisitiza msimamo wake wa kukataa shule za umma kupokea wanafunzi wanaopata mimba wakiwa katika masomo, rais aliyataka mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO) yanayowatetea kuanzisha shule kwa ajili yao.

“Nataka niwaambie, katika utawala wangu hakuna mwanafunzi mwenye mimba atakayerudi shuleni. Yapo mambo mengi ya kufanya, wanaweza kwenda Veta au wakajifunza kushona, maisha yakaendelea,” alisema Rais Magufuli alipokuwa akizungumza na wananchi wa Bagamoyo wakati wa uzinduzi wa barabara ya Bagamoyo- Msata. 

“Haiwezekani Serikali ikawa inatenga Sh bilioni 18.77 kila mwezi kwa ajili ya elimu bure halafu wanafunzi wanakwenda kufanya mambo ya ovyo. Hatuwezi kulipeleka Taifa hili katika maadili ambayo hayapo. Hizi NGO zinapata fedha nyingi zikafungue shule za wazazi, sisi tutazisajili lakini si watoto waliozaa warudi shule,” alisema. 

Uingereza yakunwa
Sera ya elimu bure kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari nchini imeigusa Serikali ya Uingereza na hivyo kuahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika masuala mbalimbali ya kimaendeleo, ikiwa ni mwendelezo wa ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo mbili.

Agosti mwaka huu, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dk. Augustine Mahiga, alieleza hayo alipokuwa akizungumzia ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza anayeshughulikia Masuala ya Afrika, Jumuiya ya Madola na Idara ya Ushirikiano katika Maendeleo ya Kimataifa.

Balozi Mahiga alisema Uingereza ni ya pili miongoni mwa wahisani wanaotoa misaada ya kimaendeleo ikiifuatiwa na Benki ya Dunia (WB).

 “Serikali ya Uingereza ni moja ya nchi inayoongoza kwa uwekezaji nchini katika biashara, viwanda na  sekta binafsi. Pamoja na kuwa zipo nchi nyingi zaidi tunazoshirikiana nazo kibiashara, Uingereza ni miongoni mwa nchi tano zinazowekeza zaidi nchini,” alisema Balozi Mahiga.

Aliongeza kuwa mbali na ushirikiano uliopo baina ya Serikali za nchi hizo mbili, Uingereza imeendelea kushirikiana na baadhi ya Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali (NGO’s), Sekta ya Afya, Elimu na mahusiano baina ya watu na watu.

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza anyeshughulikia Masuala ya Afrika, Jumuiya ya Madola na Idara ya Ushirikiano katika Maendeleo ya Kimataifa, Rory Stewart, amesema amefurahi kuja Tanzania na kupata fursa ya kutembelea baadhi ya shule Dar es Salaam na pia amefurahia Sera ya Elimu bure inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dk. John Mgufuli.

Waziri Stewart alisema kutokana na kuridhishwa na Sera hiyo, Serikali ya Uingereza itatoa msaada wa pauni milioni  140 za Uingereza kwa lengo la kusaidia katika sekta ya elimu ili kuboresha miundombinu muhimu katika sekta hiyo.

“Nimeridhishwa na Sera ya Serikali ya Elimu bure na kutokana na mwitikio mkubwa wa wazazi kuwapeleka watoto shule hali inayopelekea kuongezeka kwa idadi kubwa ya wanafunzi, tumeona nasi tushiriki katika kuboresha sekta hiyo,”  alisema Waziri Stewart.

Sunday, October 29, 2017

MIAKA MIWILI YA JPM : NI MAGEUZI MAKUBWA

Na Ibrahim malinda

IKIWA jana Oktoba 25, imetimia miaka miwili, tangu watanzania wapige kura za Uchaguzi Mkuu na kuchagua Rais, wabunge na Madiwani ambapo Dk. John Magufuli alichaguliwa kuwa Rais wa tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mageuzi makubwa yameelezwa kufanyika katika sekta mbalimbali za kimaendeleo kwa kipindi cha miaka miwili ya uongozi wake imeelezwa.

Mageuzi hayo ni pamoja na kufanikisha elimu bure kuanzia shule ya msingi hadi sekondari, ambapo hivi sasa wanafunzi wanagharamiwa kila kitu na serikali kuanzia ada za shule, mitihani, chakula, jambo ambalo kwa miaka zaidi ya 20, halikuwepo.

Kuwezekana kwa jambo hilo, kumemfanya Dk. Magufuli kuwa mmoja wa viongozi hodari walioweza kutimiza ahadi zao ndani ya muda mfupi na hata kutoa taswira kubwa ya mabadiliko ya maendeleo ambayo kwa namna moja au nyingine walikuwa hakuna.

Taarifa ilizozipata gazeti hili, zilieleza kuwa elimu bora imekuwa mkombozi na hata kufanya kila mzazi kupunguziwa majukumu ya masomo kwa watoto, ambao awali ilikuwa mtihani mkubwa kwa wananchi kushindwa kumudu gharama za masomo.

Mmoja wa mwananchi aliyezungumza na gazeti hili, Joseph Yona, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM wa Tawi la Bokorani, lililopo Temeke, alisema kuwezekana kwa elimu bure ni msaada tosha kwa wananchi, ambao kwa muda mrefu walikuwa wanashindwa kusomesha watoto wao.

“Elimu ni nyenzo ya maendeleo, anapojitokeza kiongozi anaweka jitihada kubwa katika elimu ni msaada tosha. Naifurahia kura yangu niliyoipiga kwa kuwa imesaidia kupata kiongozi bora na mwenye malengo makubwa kwa nchi,’’alisema alipokuwa anazungumza na gazeti hili.

Jamvi la Habari, lilielezwa kuwa ununuzi wa ndege sita mpya , ni uamuzi ambao unatajwa ni wa kihistoria, ambapo kwa muda mrefu nchi ilikosa ndege zake na hata kuhatarisha ustawi wa Shirika la Ndege Tanzania(ATCL), ambalo lilikuwa linaelekea kuzimu.

Kuzinduka kwa shirika la ndege ni moja ya hatua kubwa ya kukuza mapato kwa taifa lolote, hivyo inaelezwa uwepo wa ndege hizo ni hatua kubwa ya kimaendeleo, ambayo kila mtanzania anapaswa kufurahia maendeleo hayo, ambayo yamekuwa makubwa sana.

Akizungumzia fursa za uwepo wa ndege hizo, mfanyabiashara Yusuph Rashid alisema nchi kuwa na ndege zake ni hatua kubwa, hivyo kila mtanzania anapaswa kuona hii ni ufahari mkubwa ambao nchi itapata maendeleo makubwa.

“Leo hii soko la ndege ya Afrika kwa nchi za Afrika limetekwa na Kenya, pamoja na Ethiopia, hivyo nasi lazima tuwe na uhakika wa ndege zetu kwa vile Tanzania inaouwezo mkubwa wa kuwa na mashirika makubwa ya ndege, ambayo kwa namna moja au nyingine tunaouwezo huo,’’alisema.

Taarifa zaidi ilieleza kuwa ujenzi wa reli ya kisasa kwa kiwango cha stardand gauge kutoka Dar es Salaam hadi, Mwanza na Kigoma ni hatua moja kubwa ya kimaendeleo, ambapo kwa zaidi ya miaka 100 reli mpya ya kisasa ilikuwa hakuna, hivyo uwepo wa reli hiyo ni hatua moja kubwa ya kimaendeleo.

Ujenzi wa Barabara za Juu Ubungo na makutano ya Tazara, ni fursa kubwa ya ujenzi wa uchumi imara, ambayo Rais Dk. Magufuli amenuia kuiletea sifa kubwa nchi, kutokana na uwepo wa maendeleo hayo ni hatua moja kubwa ya kimaendeleo kwa nchi kusonga mbele.

Jamvi la Habari linaeleza kuwa uwepo wa mabadiliko makubwa ya kisheria katika sekta ya madini na nchi kuanza kunufaika na mabadiliko hayo, ni hatua kubwa ya kimaendeleo na hata kila mmoja kuona kuwa ufahari mkubwa wa ulinzi wa rasilimali za nchi kuwa zinalindwa kwa kiasi kikubwa.

Pia, inaelezwa katika kipindi cha miaka miwili Rais Dk. Magufuli ameweza kunipa heshima nchi kwa kuhakikisha tunalipwa zaidi ya Bilioni 700 na kampuni ya ACCACIA kutokana na kukwepa kodi.

Uwezekano wa jambo hilo ndio unafanya kuwepo kwa maendeleo makubwa ya nchi yanakuja ndani ya kipindi cha miaka mitano ya utawala wa Rais Magufuli kufanikiwa hasa kutokana na mapato ya kila mwezi kupanda maradufu.

Taarifa za Mamlaka ya Mapato(TRA), zinaeleza kuwa mapato ya nchi kila mwaka yanapanda ambapo sasa hivi kila mwezi toka utawala wa Dk. Magufuli, mapato yamefikia sh. Trilioni 1.3 tofauti na awali ilikuwa bilioni 900.

Ujenzi Bomba la Mafuta Kutoka Uganda Mpaka Tanga, ni mradi mkubwa unaotajwa kuwa na mafanikio makubwa kwenye utawala wa Rais Magufuli kwa kuwa utaweza kutengeneza ajira zaidi ya milioni mbili pamoja na kuipa mapato makubwa nchi.

Uwezekano wa mradi huo, ambao unatajwa kuwa moja ya miradi mikubwa kufanyika nchini, unazidi kueleza mafanikio ya utawala wa Rais Dk. Magufuli kuwa utakuwa salama na maendeleo makubwa kwa nchi.

Pia, inaelezwa udhibiti wa fedha za umma, unazidi kumpa heshima Rais Dk. Magufuli kutokana na aina ya utawala wake kuheshimu fedha za wananchi katika utekelezaji wa miradi mbali mbali nchini.

Jamvi la Habari lilielezwa kuwa ifikapo 2020 zaidi ya asilimia 95, mijini na vijini kutakuwa na uhakika wa maji safi na salama kutokana na utekelezaji wa miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa fedha za ndani pamoja na wahisani waliolizika na utawala imara wa Rais Dk. Magufuli.

Katika kipindi cha miaka miwili ya Rais Dk. Magufuli huduma mbalimbali za afya zimeboreshwa ikiwemo ununuzi wa vifaa tiba na huduma kama, MRI, CT-SCAN zanunuliwa kwa mafanikio makubwa.

Pia Rais Magufuli amefanikiwa kudhibiti upotevu wa Mapato Bandarin pamoja na kufanikiwa kuimarisha miundombinu ya barabara sehemu mbali mbali ya nchi.

Monday, October 23, 2017

BREAKING NEWS:- DKT. KIGWANGALA ATEMA CHECHE LIVEEEE

https://4.bp.blogspot.com/-oiMWgSB8QiU/V8_WRSqCVbI/AAAAAAADjag/U93sv9X_0nQee8C8tPcpeV7HFZFWcnxBgCLcB/s640/st0F40Nn.jpgDKT. KIGWANGALLA AMWAGA CHECHE, AFUTA UTARATIBU WA UTOAJI WA VIBALI VYA UWINDAJI WA KITALII, AAPA KUTOYUMBISHWA NA RUSHWA NA FITNA
NA HAMZA TEMBA - WMU - DODOMA
...................................................................................
Katika kile alichoeleza kuwa ni kuimarisha sekta ya maliasili na utalii iweze kutoa mchango unaostahili kwa jamii na taifa kwa ujumla, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla amesitisha utaratibu wa kuhuisha upya vibali vyote vya makampuni ya uwindaji wa kitalii ambavyo vilitolewa mwaka huu mwezi Januari ili kupisha utaratibu mpya wa utoaji wa vibali hivyo kwa njia ya mnada.

Dk. Kigwangalla ametangaza uamuzi huo jana mjini Dodoma katika mkutano alioutisha wa wadau wa sekta ya maliasili na utalii ambao ulilenga kukusanya maoni, kero na kujadili changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo muhimu nchini kwa ajili ya kuzitafutia utatuzi wa haraka.

“Kwa mamlaka niliyopewa na sheria ya wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009, nimeamua bila kushawishiwa na mtu yeyote yule wala kushauriwa na mtu yeyote yule zaidi ya kusikiliza tu ushauri wa kitaalamu na ushuari wa ndugu yangu Mhe.  Naibu Waziri, lakini  sasa hivi ninavyotamka haya sijamshirikisha mtu yeyote yule, nimeamua kwa mamlaka yangu, nasitisha vibali vyote  vya uwindaji wa makampuni ambavyo vilitolewa mwaka huu mwezi Januari kwa maana ya ‘kurenew’ (kuhuisha).

“Nasitisha ili kupisha mchakato wa kutengeneza taratibu mpya za kuendesha ugawaji wa vitalu kwa njia ya mnada, tunataka twende kwenye ‘auction’ (mnada) ya vitalu, na auction (mnada) iwe ya wazi, iwe na faida kubwa  zaidi, na natoa siku sitini utaratibu huo uwe umekamilika ili tuweze kuendesha ‘auction’ (mnada) kabla ya muda wa kuanza kwa awamu ya miaka mitano ambayo ni january 2018 mpaka 2022.

“Kwahiyo ndani ya siku sitini, wataalam mkae mniletee utaratibu wa namna bora zaidi ya uwazi inayotoa haki ya kugawa vitalu lakini pia yenye faida kubwa zaidi kama tunavyoelekezwa na mpango wa taifa wa miaka mitano kwamba ni lazima vitalu vyote vifanyiwe ‘auction’ (mnada)”. alisema Dk. Kigwangalla.

Alisema utaratibu huo hautahusisha vitalu vilivyopo kwenye maeneo yenye migogoro ya ardhi kwa sasa mpaka pale migogoro hiyo itakapomalizika.

“Ni mwiko kugawa vitalu kwenye maeneo yenye mgogoro, kuna maeneo kama vitalu vilivyopo Loliondo, kuna mgogoro, ni mwiko kugawa vitalu, kuna maeneo kama Lake Natron kuna mgogoro, mwiko kugawa vitalu, mpaka tutatue migogoro kwanza, Kama kuna mtu alipewa kibali huko nyuma ajue hicho kibali cha renewal  kimekufa leo na mimi ndio nimekiua” alisema Dk. Kigwangalla.

Kuhusu uwindaji wa Wenyeji kwenye maeneo ya wazi uliosimamishwa kwa muda wa miaka miwili sasa, Dk. Kigwangalla alitoa muda wa siku sitini kwa watendaji wa wizara yake kukamilisha masharti mapya ya uendeshaji wa biashara hiyo na kuyawasilisha kwake aweze kuyasaini ili kufungulia biashara hiyo.

“Natoa siku sitini, wataalam wetu mnaohusika na utoaji wa vibali vya uwindaji wa wenyeji mkamilishe masharti mapya mniletee nisaini tutoe vibali, hatuwezi kuzuia wenyeji wanufaike na rasilimali ambazo ziko huko vijijini alafu tukaruhusu makampuni ya watu kutoka nje kuja kuwinda wakaondoka na nyama, ni lazima tutoe haki kwa wazawa kama wapo wanaovunja masharti sisi tudhibiti na tusimamie sheria” alisema Dk. Kigwangalla.

Wakati huo huo, Waziri Kigwangalla amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Mej. Jen. Gaudence Milanzi kuwasiliana na Msajili wa Hazina kwa ajili ya kuanza mchakato wa kuzirudisha serikalini hoteli za kitalii kumi zilizobinafsishwa miaka 1990 kufuatia kushindwa kutimiza masharti ya mkataba wa uendeshaji.

“Niagize Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii uwasiliane na mamlaka ambayo ina dhamana ya kushikilia mali zilizokuwa za Serikali ambazo ziliuzwa kwa maana ya msajili wa hazina, umueleze nimetoa agizo kwamba hizi hoteli zote ambazo zimekiuka masharti na hivyo kuathiri utendaji wa sekta ya utalii nchini na hivyo kuathiri uchumi mpana wa taifa letu, zichukuliwe na zirudi kuwa mali ya serikali ili serikali ipate fursa ya kuzitangaza upya na kutafuta waendeshaji wapya watakaoweza kuendesha hoteli hizi  kwa tija na ufanisi kwa maana ya kukuza sekta ya utalii ambayo inachangia asilimia 17 ya pato la taifa.

“Nimetoa agizo hoteli hizi 10 ambazo zimeshindwa kukidhi masharti ya mikataba ya mauziano, mchakato wa kuzirudisha Serikalini uanze mara moja na ukamilike ndani ya siku sitini.

Alisema kumekuwepo na changamoto kubwa ya uhaba wa vyumba katika sekta ya utalii hali iliyosababishwa na ubinafsishaji wa hoteli 17 za Serikali uliofanywa miaka 1990 kwa nia njema ya kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa hoteli hizo kupitia sekta binafsi lengo ambalo halikufikiwa kwa baadhi ya hoteli hizo.

“Baada ya kufanya uchunguzi katika hoteli zote 17 tulizouza ni saba tu zinafanya vizuri, hoteli zinazofanya vizuri na zimekidhi masharti yote ambayo yalikuwepo kwenye ile mikataba ni Kilimanjaro Hotel, Kunduchi Beach Hotel, Mt. Meru Hotel, New Africa Hotel, New Safari Hotel, Mafia Highland Hotel na Hotel 77.

“Hoteli 10 zimeshindwa kukidhi masharti ya mikataba ya mauziano na mwaka ulioisha Serikali ilifanya uchunguzi kwenye hoteli nyingine nne kati ya hizo 10 ambazo ni Robo Wildlife Lodge, Seronera Wildlife Lodge, Ngorongoro Wildlife Lodge na Lake Manyara Hotel, na zote zilionesha zipo chini ya kiwango na hazikidhi mahitaji.

“Kwa kuwa watu hawa wamekiuka masharti ya ubinafsishaji kama walivyopewa wakati wananunua hizo hoteli ni wakati muafaka sasa kwa Serikali kuvunja hii mikataba kuzichukua hizi hoteli na kuzibinafsisha kwa watu wengine watakaoweza kuziendesha kwa faida lakini pia kuziendesha kwa tija zaidi” alisema Dk. Kigwangalla.

Awali akijibu baadhi ya hoja za wadau wa mkutano huo kuhusu wizara yake kuwa na vishawishi vingi vya rushwa na fitna ambazo husababisha viongozi wengi kutodumu kwenye nafasi zao, Dk. Kigwangalla alisema kamwe hatoruhusu hali hiyo ijitokeze kwa kuwa hata aliyemteua anamjua vizuri kuwa ni muarobaini wa changamoto hizo.

“Mimi nipo hapa kwenye hiki kiti, na nitakuwepo kama sababu ni hiyo ya maslahi, Mimi sihongeki, sinunuliki, na sishawishiki, najua hata aliyeniweka hapa ananijua vizuri, kwahiyo alivyoniweka hapa alishajua hii ni dawa, muarobaini.

“Watu wote humu ndani tuna njaa, lakini njaa yangu nabaki nayo mwenyewe, bora nife kwa heshima zangu kuliko kuaibika na kudharaulika kwa kuchukua rushwa ama kwa kutokutenda haki ama kwa kumuonea mtu.

“Hilo nina uhakika nalo, kwa maana ya rushwa, maslahi ya kibiashara hapana, hutonikuta mimi huko, na kama kuna mdau mmoja anadhani kuna siku anafkiria anaweza kuja kuongea na mimi kwa maslahi binafsi akaweka mbele mazingira ya rushwa, sana sana ataona nimemuaga na kikao chetu kimeishia hapo, kwahiyo ukija kwangu njoo na ishu ambayo ipo straight maslahi ya umma yapo ndani yake utaraibu wa kisheria upo”. Alisema Dk. Kigwangalla.

Miongoni mwa maagizo mengine aliyoyatoa kwenye kikao hicho kwa watendaji wa wizara yake ni kuandaa taratibu za kuanzishwa kwa mwezi maalumu wa kuadhimisha utamaduni wa Mtanzania (Tanzania Heritage Month), Makumbusho ya Marais wa Tanzania (Presidential Museum) na Utalii wa Mabasi kwa Miji ya Dar es Salaam na Arusha (Dar Bus Tour/ Arusha Bus Tour) ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa watalii katika miji hiyo.

Katika mkutano huo wadau wa maliasii na utalii walipata fursa ya kutoa maoni, mapendekezo ushauri na kero mbalimbali wanazokumbana nazo katika sekta hiyo ambazo ziliahidiwa kufanyiwa kazi kwa haraka na Waziri Kigwangalla.  Miongoni mwa ushauri na mapendekezo waliyotoa ni pamoja na kuanzishwa kwa mamlaka moja inayosimamia rasilimali za misitu nchini na kufunguliwa kwa biashara ya kusafirisha viumbe hai nje ya nchi.

Mkutano huo wa siku moja ulihudhuriwa na viongozi wakuu wa Wizara ya Maliasili ambao ni Naibu Waziri, Mhe. Japhet Hasunga, Katibu Mkuu, Mej. Jen. Gaudence Milanzi, Naibu Katibu Mkuu, Dk. Aloyce Nzuki, Wakurugenzi wa Idara na Wakuu wa taasisi zilizopo chini ya Wizara hiyo.

Wengine ni wadau zaidi ya 200 kutoka sekta mbalimbali ya maliasili na utalii ambao ni wawakilishi kutoka vikundi, taasisi, vyama na vyombo mbalimbali vinavyoshughulika na utoaji wa huduma katika sekta ya utalii, wanyamapori, misitu na nyuki pamoja na waandishi wa habari.