WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Sunday, August 27, 2017

USALAMA ASILIMIA 100 KIBITI

Viongozi na wananchi waliolazimika kukimbia Kibiti baada ya kuwapo na matukio ya kila mara ya kuuawa kwa wenzao huku wahalifu wa unyama huo wakiwa hawafahamiki, wameendelea kurejea katika maeneo yao baada ya hali ya usalama kuendelea kuimarika siku baada ya siku imefahamika.

kuimarika huko kwa hali ya usalama katika siku za hivi karibuni kulikotokana na operesheni mbalimbali zinazoendelea kufanywa na vyombo vya kulinda usalama wa raia na mali zao kumewapa imani wengi wao ambao sasa wameanza kurejea, ingawa imefahamika kuwa kasi ya kurudi kwa baadhi yao imekuwa ni ya kuvizia, kuashiria kuwa wapo ambao bado wamejawa na wasiwasi.

Akizungumza hivi karibuni, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti, Alvela Ndabagoye, alisema kuwa baada ya ombi lake la wiki iliyopita la kuwataka viongozi na watendaji kurejea kazini ili waendelee kutoa huduma kwa wananchi, sasa hali imekuwa ya kutia moyo kwa sababu wengi wameitikia wito huo na kurejea.

"Tumefanikiwa kuwarejesha (watendaji) wote 16 ambao walikimbia ofisi zao kutokana na kuwapo na matukio ya mauaji, hali sasa imekuwa nzuri kwa wananchi kutokana na kuendelea kupata huduma kutoka kwa watendaji hao,'' alisema.

Aliongeza kuwa, watendaji hao walimwelewa na wakakubali kurudi katika vituo vyao vya kazi na hivi sasa wanaendelea kutoa huduma kama kawaida.

Mkurugenzi huyo alisema pamoja na kurejea kazini, bado baadhi ya watendaji wana wasiwasi kwani wamekuwa wakifanya kazi kwa muda mfupi na kurejea nyumbani.

Alisema pamoja changamoto za kiusalama zilizokuwapo katika wilaya hiyo, watumishi wa kada zingine waliendelea kutoa huduma kwa wananchi.

Wiki iliyopita katika kikao cha robo mwaka cha Baraza la Madiwani kilichofanyika Kibiti na kuhudhuriwa na madiwani, wakuu wa idara pamoja na wananchi, Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Milongo Sanga aliwaondoa hofu watendaji wa vijiji na kuwataka warejee ofisini kwao ili kuendelea kutoa huduma kwa jamii kutokana na hali ya kiusalama kuimarika.

"Tunawaomba wenyeviti wa vijiji warudi kazini kuendelea na utoaji wa huduma kwa wananchi kwani kwa sasa hali ya Kibiti imeimarika na hakuna matatizo yoyote," alisema Sanga.
Wilaya za Kibiti, Rufiji na Mkuranga mkoani Pwani, zilikumbwa na mauji mfululizo ya kikatili lakini hivi karibuni, jeshi la polisi lilitangaza kuwa usalama umeimarika na sasa wananchi wanapaswa kuendelea na shughuli zao bila hofu.

Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro, alitangaza vilevile kuwa Polisi imewaua watu 13 wanaohusishwa na mauaji hayo wakati wakiwa katika harakati za kuwadhibiti.

Katika tukio mojawapo la mauaji yanayoendelea eneo hilo, askari polisi wanane waliokuwa kwenye gari wakitoka lindo waliuawa kwa risasi Aprili 13 mwaka huu walipofika eneo la Mkengeni. Kata ya Mjawa Wilaya ya Kibiti.

Katika tukio hilo, majambazi hao walipora bunduki saba ambazo ni SMG nne na Long Range tatu zikiwa na risasi zake.

Katika tukio hilo askari mmoja alijeruhiwa na baadaye polisi walitangaza kuua wahalifu wanne waliodaiwa kuwa majambazi baada ya kubaini maficho ya muda katika majibizano ya risasi.

Zawadi ya Sh. milioni 10 ilitangazwa na IGP Sirro kwa mtu yeyote atakayefanikisha kukamatwa kwa wahusika wa mauaji hayo.

Kabla ya kutangazwa kwa zawadi hiyo ya IGP, Polisi mkoani Pwani ilikuwa imetangaza zawadi ya Sh. milioni tano kwa mwananchi yeyote ambaye atafanikisha kukamatwa kwa watuhumiwa 12 wa mauaji ambao ilidaiwa hujihusisha na mtandao wa mauaji hayo.

Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Sanga Lyanga, aliwaambia waandishi wa habari Mei 22, kuwa jeshi hilo limepata picha za baadhi ya watuhumiwa na fununu za mahali wanapopenda kutembelea mara kwa mara.

Kamishina Lyanga aliwataja watuhumiwa hao pamoja na mwanzilishi wa mtandao huo wa mauwaji kuwa ni Abdulshakur Ngande Makeo, Faraja Ismail Nangalava, Anaf Rashid Kapera, Said Ngunde na Omary Abdallah Matibwa.

Wengine ni Shabani Kinyangula. Haji Utaule, Ally Utaule, Hassan Upinda,Rashid Salim Mtulula,Sheikh Hassan nasr Mzuzuri na hassani Njame.

Mfululizo wa mauji hayo ulianza Mei mwaka jana katika tukio la kupigwa risasi kwa Mwenyekiti wa kijiji cha Nyambungu, Saidi Mbwana.
Kadharika, hivi karibuni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama mkoani Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo, amewahakikishia wananchi kuwa hali ya usalama wilaya ya Kibiti na Rufiji ipo shwari. Aidha amesema jeshi la polisi linaendelea na oparesheni mbalimbali za kuwasaka wahalifu wanaochafua mkoa na taifa.
Aliyasema hayo, kufuatia habari zinazoendelea kusemwa na kuandikwa katika baadhi ya vyombo vya habari kuhusu mambo yanayoendelea kwenye wilaya hizo. Mhandisi Ndikilo, aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa polisi waliopo kwenye oparesheni hiyo na kuacha kukimbia miji yao kama wanajiamini sio wahalifu.

"Kumekua na taarifa zinazoendelea kuandikwa suala ambalo mkoa haujawahi kutoa taarifa zaidi ya tukio la mauaji ya vifo nane iliyotokea april 13 na kukemea usafiri wa pikipiki ifikapo saa 12 jioni " alisema. Alibainisha kwamba, endapo kutakuwa na tukio ama jambo litakalojitokeza serikali ya mkoa, wilaya, jeshi la polisi litatolea ufafanuzi.

Mwenyekiti huyo wa kamati ya ulinzi na usalama ambae pia ni mkuu wa mkoa huo, alieleza, kuwa sasa vyombo vya dola vinawasaka watu waliojihusisha na mauaji ya wenyeviti wa vijiji, vitongoji na polisi . "Jeshi la polisi ama serikali haiwezi kumwonea mtu yoyote kwani inafanywa kwa kuzingatia sheria"alisema.

Mhandisi Ndikilo alisema jeshi la polisi linafanya kazi yake kwa weledi na kazi yake kubwa ni kulinda amani ya wananchi na mali zao. “Nawaombeni wananchi msiwe na hofu juu ya operesheni hiyo na hakuna haja ya kukimbia makazi yao kwani kuna taarifa kuwa kuna watu wamehama kwenye nyumba zao na kukimbia,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa watu wanaokimbia wanatia mashaka, hawana sababu ya kukimbia nyumba zao na familia zao kwani wanaotafutwa ni wahalifu na si raia wema. Mhandisi Ndikilo, alisema wananchi wanapaswa kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola ili viweze kufanya kazi zake ipasavyo.
Aliwatoa hofu watu wote wanaofanya shughuli zao kwenye wilaya hizo kutokuwa na wasiwasi kwani ulinzi umeimarishwa

MAKADA CHADEMA WAMPONDA LISSU.


Wadai Kuchoshwa na tabia yake ya Kuropoka,  Kukurupuka

Waitaka Serikali, Polisi wamdharau wasimpe Kiki

Wasema dawa ni kumpuuza, Kumkamata  ni kumpa sifa asizostahili.

wamuhusisha na Mbio za Urais CHADEMA 2020

Makada na wanachama sita wa CHADEMA wanaotoka wilaya ya Ikungi mkoani Singida ambao ni wananchi na wapiga kura wa jimbo la singida mashariki linaloongozwa na Mbunge Tundu Lissu ambaye pia ni mwanasheria mkuu wa chama hicho na mnadhimu wa kambi rasmi ya upinzani Bungeni mheshimiwa Tundu Lissu wamemjia juu mbunge wao na kumtaka abadilike mara moja na kuacha kukiingiza chama kwenye migogoro isiyo ya lazima vinginevyo ndoto yake ya kuwa mgombea urais wwa chama hicho katika uchaguzi ujao wa mwaka 2020 ataisikia kwenye bomba.

Makada hao, Shaaban Kipengwa, Isimtwa Joseph, Kulwa Malimbile, Swabaha Jumanne, Mughwai Cripin na Omar Sadiki wamesema maneno hayo katika mahojiano yaliyofanywa kwa nyakati tofauti na gazeti hili kutaka kujua juu ya mtazamo wao dhidi ya mbunge wao na mwanachama mwenzao kwa yale yanayomtokea hivi sasa.

‘’Kwa kweli Lissu ni alikuwa ni kiongozi mzuri san asana sana, hapa jimboni angeweza kuwa hata mbunge kwa kipindi cha maisha yake yote, tatizo tu siku hizi ameacha kutumia akili, si Lissu yule tuliyemchagua 2010, amebadilika sana, sasa hivi Lissu ni bingwa wa kuropoka ropoka tu. Kwa kifupi Lissu wa sasa ni  Mkurupukaji’’ alisema Kipengwa.

Naye bwana Malimbile alionyesha masikitiko yake kwa serikali na jeshi la polisi namna wanavyomchukulia na kuwataka wampuuze na kumdharau na si kuendelea kumpa sifa mawazo yaliyoonyesha kufanana kabisa na yaliyotolewa na Swabaha, Mughwai na Sadiki.

‘’Serikali yetu ama inajua au haijui, Lissu siyo mtu wa kumjibu, atawavuruga tu hana lolote alijualo la maana, kama serikali ingempuuza Lissu nahakika asingehangaika na hayo magazeti huko mjini, angekuja huku Ikungi tuchote nae maji ya visima, tatizo serikali inampa kiki’’. Alisema Mughwai

‘’ningekuwa mimi ni kiongozi wa polisi hapa nchini, Lissu sio mtu wa kumkamata, Lissu anachokifanya ni kama motto mdogo anayekutishia mzazi wake kwamba usipompa kitu Fulani  ni atajikojolea, alikuwa ni mtu wa kumpotezea tu. Kumkamata kamata huku ndiko anakokutaka ili ajionyeshe kwamba yeye ndio mpinzani sahihi wa serikali’’. Alinukuliwa

Isimwa aliongeza kuwa polisi wanapomkamata Lissu wanakuwa hawajamkomoa yeye wala kuisaidia serikali bali wanakuwa wamemuongezea sifa na kutimiza sehemu ya malengo yake ambayo ni kuendelea kuonekana anapambana na serikali na anakamatwa kamatwa kila mara.

 ‘’Polisi wangeachana nae tu huyu jamaa, hii kila siku sentro (Mahabusu), mara mahakamani kasha anapata dhamana haimuathiri inampa kiburi na inamjenga, inamfanya ajione kufanikiwa kirahisi mipango yake huku sisi jimboni tumekwama’’.

Kadharika wanachama hao wamemuomba mbunge wao huyo kutembelea jimbo lao hilo hata mara moja kwa mwezi na kumtaka aachane na habari za kukaa Dar es salaam na kuwatelekeza wananchi na wapiga kura wake bila hata kufanya jitihada za kushirikiana nao katika kutatua changamoto za kimaendeleo

‘’Kama unavyoona hii ndio hali ya maisha yetu hapa jimboni, Maisha magumu, Huduma za kijamii bado hazijatengemaa, AFya na huduma zake zipo duni, barabara ndio kama ulivyojionea mwenyewe hazipitiki kirahisi, vijana hawana ajira lakini bado mbunge wetu kutwa kucha kushinda mahakamani na kwenye magazeti na TV, sisi hatukumchagua na kumpigania awe mshinda mahakamani, tulimchagua awe mwakilishi wetu kama alivyojitahidi kuwa katika awamu yake ya kwanza 2010’’. Aliongeza Isidori

Taarifa za uhakika ambazo gazeti hili linazo kutoka miongoni mwa viongozi wakuu wa chama hicho ni kuwa, anachokifanya Lissu hivi sasa hakina Baraka za viongozi wenzake bali ni jitahada zake binafsi za kile walichokiita maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao wa ndani ya chama na ule mkuu wa serikali.

‘’viongozi wote wanajua kuwa Lissu ana ndoto mbili kuu hivi sasa, moja kama itakuwa rahisi kwake, ni kugombea nafasi Fulani kubwa ndani ya chama ili alete mabadiliko ya kimfumo na kiutendaji ndani ya chama kama mwenyewe anavyo amini na nyingine ni ile yam zee Lowassa ya kugombea Urias 2020’’. Anasema msiri wetu ambaye ni mmoja wa wakurugenzi wa chama hicho

‘’Lissu mpaka sasa anaamini kwamba yeye ni mtu sahihi kabisa kupambana na Magu (Dkt. John Magufuli) kwenye uchaguzi ujao, anasema Lowassa hawezi tena kumvaa Magu wala Mbowe hatoshi. Ndio maana kila mara anaendelea kuji-positioni (Kujipanga). Tusubiri tuone itakavyokuwa’’. Kiliongeza chanzo hicho

Katika toleo letu lililopita, Gazeti hili tulielezea kwa undani kuwa Kitendo cha Mwanasiasa na Mbunge wa Ikungi kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA ambaye pia ni mwanasheria mkuu wa Chama hicho Tundu Lissu kuishambulia serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli na hivi karibuni kuihusisha na kile alichokiita kukwama kwa ndege zilizonunuliwa na serikali ya Tanzania nchini Canada kimemfanya mbunge huyo kupuuzwa na watu makini huku akihusishwa na kufilisika kisiasa.

Akiongea na Gazeti hili Kaimu Mkurugenzi wa muungano wa Taasisi zinazojihusisha na masuala ya utetezi wa Rasilimali, Haki na Utawala wa Sheria uoutwa ULINGO WA KATIBA Bwana Ally Bushiri amesema hakutarajia kuona kama maneno anayoyasikia yangeweza kutamkwa na mwanasiasa huyo aliyejipambanisha kama mtetezi wa wanyonge na mzalendo.

‘’huwezi kujiita Mzalendo ama mtetezi wa wanyonge halafu ushiriki kuihujumu serikali, hata kama inaongozwa na kiongozi usiyempenda kiasi gani, haiwezekani’’. Alisema Bushiri

‘’kila siku Lissu anaibuka na kashfa mpya, na kashfa zote ni kumchafua Rais tu, hata kama anajiandaa kugombea Urais 2020 lakini si kwa mtindo huu….Lissu lazima afahamu kwamba Waziri yeyote yule hapa Tanzania, Afrika na Duniani hana Mamlaka ya Kusaini Mkataba wa kizabuni kama ujenzi, na ndio maana kunakuwa na mamlaka za manunuzi ambazo ni huru na haziingiliwi na taasisi yoyote, na ndio maana Lowassa alipojaribu kuingilia kwenye zabuni ya Richmond alikwenda na Maji’’. Alisisitiza bwana Ally.

Aidha mkurugenzi huyo ameongeza kuwa haikuwa rahisi na isingewezekana kwa kile alichokisema Lissu kuwa Rais Magufuli alipokuwa waziri aliweza kuvunja mkataba na kampuni moja ya kigeni jambo ambalo kisheria waziri hana mamlaka ya kufanya hivyo kutokana na ukweli kwamba yeye si sehemu ya mkataba wa ujenzi ambayo kwa barabara kubwa hapa nchini husimamiwa na Wakala wa Barabara nchini maarufu kama TANROADS.

‘’Lissu angeweza kusema kuwa sisi kama nchi tunadaiwa, na mmoja kati ya wadeni wetu amekosa uvumilivu ameamua kuchukua hatua kali zaidi, wala haina maana ya ziada kusema tunadaiwa deni lililosababishwa na Fulani, serikali haifanyagi kazi namna hiyo dunia nzima, labda wao Chadema kama ndivyo wanavyoongozana hivyo’’. Alisisitiza

Bushiri aliongeza kuwa Tanzania kwa mujibu wa taarifa za kifedha mpaka sasa inadaiwa zaidi ya Trilioni 40 na kwamba haijaanza kukopa leo wala jana na kamwe haiwezi kuacha kukopa kesho wala kesho kutwa kwa kuwa inafuata taratibu zote za kisheria na kifedha.

‘’Mwalimu Nyerere alikopa na akadaiwa, Mzee Mwinyi naye kakopa, Rais Mkapa alikopa na akadaiwa, Mzee Kikwete naye Kadharika, na wote hawa walikopa na kulipa na kukopa na hata Magufuli amekopa na atalipa na atakopa, sasa shida iko wapi?...Mbona Marekani wanadaiwa, Uingereza Wanadaiwa..nchi zote unazozijua kubwa kwa ndogo hapa uniani zinadaiwa. Alisisitiza

Aidha bwana Bushiri amewataka watanzania kutomkubalia na kumuamini Lissu kwa haraka bila kupima jambo analowaambia kutokana na ukweli kwamba mwanasiasa huyo hachelewi kugeuka na kubadili msimamo wake bila kujali jana amesema nini.

‘’Lissu sio wa kumuamini sana. Leo anaweza kusema hivi kesho vile, ni mjanja mjanja, ndio maana mwaka 2007 Lissu alituambia watanzania tumchukie Lowassa kwa kuwa ni FISADI  lakini mwaka 2015 akatuambia tumchague Lowassa kuwa Rais wa Tanzania vinginevyo tuthibitishe UFISADI wa Lowassa…hivyo anaweza siku moja akatuambia tuthibitishe haya anayoyaropoka leo…ili umuamini Lissu inakubidi uwe na akili kama zake ’’. amenukuliwa Bushiri

Hivi karibuni  serikali imetoa tamko na kueleza kuwa baadhi ya wanasiasa wapo katika mkakati wa kuhujumu mipango ya maendeleo na usalama wa nchi ambao wameshiriki kuchochea kuwekwa zuio la ndege mpya ya kuwasili nchini.

Jamvi la Habari limepata taarifa ya serikali iliyosema kuwa licha ya uwepo wa zuio hilo, hatua  za kidiplomasia  na za  kisheria  zimeanza  kuchukuliwa  ili kulimaliza na ndege hiyo itawasili nchini.

Zuio hilo la mahakama linalodaiwa kuwekwa na kampuni moja ya ujenzi nchini Canada, ikiidai serikali fedha kufuatia kuvunjwa mkataba wa ujenzi wa moja ya barabara iliyokuwa ikijengwa nchini.

Hatua hiyo iliyochochewa na wanasiasa wanaoendeleza hujuma   dhidi ya maendeleo ya nchi, imesababisha ndege ya tatu aina ya Bombardier Q 400, kuzuiwa nchini Canada.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa , Dar es Salaam na Mkurugenzi Msaiadizi wa Idara ya Habari-Maelezo, Zamaradi Kawawa, alisema serikali inawaomba  Watanzania  kutokuwa  na wasiwasi kuhusu suala hilo.

Alisema serikali ilikuwa na fununu kwamba kuna baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa, wanaendeleza juhudi za kuhujumu jitihada za Rais Dk. John Magufuli, za kuwaletea Watanzania  hasa wanyonge maendeleo.

“Walikwenda  kufungua madai  kuwa, serikali  inadaiwa  na kwamba ndege  hiyo  ishikiliwe, watu hawa hawana  uhalali wowote  wa kufanya hivyo,  na ni matapeli  ambao wamesukumwa  na baadhi ya viongozi  wa kisiasa  wasioitakia mema  nchi.''alisema

Aliongeza kuwa “Kwa kuwa serikali ilishapata  fununu  kwamba kuna  baadhi ya  viongozi  wa chama  cha siasa  wanampango  huo, sasa  watu hao wamejiridhisha  hadharani,  kwamba wao  ndio wako nyuma  ya pazia  la  kuhujumu  jitihada  za serikali  kwa maslahi yao ya kisiasa,” alifafanua.

Kwa mujibu wa Zamaradi alisema serikali ya  Dk. Magufuli itawahakikishia  Watanzania  kuwa, ndege  itakuja na wanaokwamisha  jitihada hizo  watapanda ndege hizo na ndugu zao  na wafuasi wao.

Zamaradi alibainisha kuwa, kundi hilo limekuwa likichochea wafadhili wasitishe misaada nchini, wakidhani kufanya hivyo ni kukomoa serikali.

Aliongeza kuwa pia serikali inafununu kwamba watu hao wanaohujumu jitihada za kimaendeleo, wanahujumu hata hali ya usalama wa raia, hivyo inaendelea kufuatilia kwa makini.

“Tunachojifunza kama serikali, hivi misaada isipotolewa anayekomolewa ni Rais Dk. Magufuli?. Au ni Watanzania wanyonge ambao wangekosa dawa, huduma za maji na umeme.

Aliongeza “Lakutia faraja ni kwamba pamoja na jitihada hizo, washirika wa maendeleo wameongeza kasi ya ushirikiano na serikali inayoongozwa na Rais Dk. Magufuli,”.

Alisema yeyote mwenye uchungu na nchi yake angepambana ili jambo linalohusu maslahi ya taifa, likiwemo la kununua ndege lisikamwe na kama kuna mkwamo, ashiriki kukwamua badala ya kushabikia.

Kauli ya Kaimu Mkurugezi huyo wa Maelezo, imefanana na kauli mbalimbali za wananchi, walioeleza kuwa Lissu amekuwa akipotosha mambo mengi, na umefika wakati wa kuchukuliwa hatua kali za  kisheria.

Jacob Agustino, ambaye ni mkazi Temeke Mtongani, alisema huyu mtu anapaswa kuangaliwa kwa umakini mkubwa hasa kutokana na kujifanya anajua sheria na mwisho wa siku anafanya mambo mengi ya ovyo.

Alisema kuna wakati alikuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha Tanzania yote ijue kuwa Waziri Mkuu Mstaafu, Edward Lowassa ni fisadia namba moja nchini na badala ya siku amekuwa mstari wa mbele katika kumsifia na kumfanya aonekane ni mtu safi.

"Watanzania tuweni makini, serikali inafanya kazi nzuri chini ya Rais Dk. John Magufuli,ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kila linalofanywa linafanywa kwa maslahi ya umma,''alisema.

Hivyo, alisema kila mwananchi mpenda maslahi anapaswa kuwa pamoja na Rais Dk. Magufuli kwa kuwa katika kipindi kifupi ameipa hadhi nchi kuwa na ndege zake zenyewe na hatimaye kuwa na mafanikio katika usafiri wa anga. 

ACT WAZALENDO ILIVYOITINGISHA MWAZA


 Ni katika Mkutano wao mkuu wa Kidemokrasia kukutanisha wanachama, wananchi na viongozi 

 Zitto Kabwe Aunguruma, Azungumzia Uchumi, Kilimo na Demokrasia

Na . Ibrahim Malinda
Zitto Zuberi Kabwe, Kiongozi wa chama cha ACT WAZALENDO juzi aliwaongoza wanachama wa chama hicho katika kuazimisha mkutano wao mkuu wa kidemokrasia wa tatu tangu kuanzishwa kwa chama hicho mkutano uliofanyika mkoani mwanza katika ukumbi wa hotel ya Monarch iliyopo jijini humo.
Ifuatayo ni hotuba iliyosomwa na kiongozi huyo wa chama ambaye pia ni mbunge wa jimbo la kigoma mjini.


Ndugu Watanzania.
Ndugu Wanachama wa Chama cha ACT Wazalendo na washiriki wa Mkutano wetu wa mwaka wa Kidemokrasia hapa Mwanza.

Nawasalimu kwa salaam za kizalendo na kuwakaribisha katika Mkutano wetu wa mwaka 2017. Huu ni Mkutano wetu wa pili wa Kidemokrasia Kwa mujibu wa Katiba ya chama chetu. Agosti mwaka jana tulikuwa Dar es salaam katika Mkutano wa Kwanza wa Kidemokrasia, ambapo tulizungumzia kwa undani juu ya suala la Katiba mpya. 

Mwaka huu mwezi Machi tulikuwa na Mkutano Mkuu wa kidemokrasia maalumu jijini Arusha kuadhimisha miaka 50 ya Azimio la Arusha, kujadili Ujamaa pamoja na umuhimu wa Azimio la Tabora la chama chetu linalohuisha Azimio la Arusha. Leo tupo hapa Mwanza katika Mkutano wa Pili wa Kidemokrasia kuzungumzia umuhimu wa Uhuru wa Fikra, Mawazo na Misingi ya Demokrasia. 

Nina furaha kubwa kwamba pamoja na upya wa chama chetu tumeweza kuendeleza bila kukosa utekelezaji wa Katiba yetu kwamba kila mwaka wanachama wawe na nafasi ya kukutana na viongozi wa chama na wananchi wengine kujadili hali ya nchi yetu kiuchumi, kisiasa na kijamii. Tusiache utamaduni huu kwani ni utamaduni unaoimarisha zaidi Chama na kuweka karibu Viongozi wa Chama na na wanachama; Chama na wananchi; Chama na wadau wake mbalimbali. 

Mkutano huu wa Demokrasia ni utaratibu unaotoa fursa ya moja kwa moja kwa wanachama kutuhoji Viongozi wao, na kushauri juu ya namna njema ya kuendesha siasa zetu. Ni ishara ya kilele cha Demokrasia ya chama chetu. Nawapongeza Sana wanachama na wananchi wote mlioweza kushiriki nasi leo. Nawatakia mjadala wa kina na wenye manufaa Kwa nchi yetu na bara la Afrika. 

Mwaka 2015 wakati wa uzinduzi wa Azimio la Tabora tulizungumza kwenye hotuba ya Tabora kuhusu changamoto ambazo nchi yetu ilikuwa nazo na inawezekana bado inazo . Katika Hotuba ile ambayo imechapishwa kwenye andiko la Azimio la Tabora tulianisha, nanukuu "Wananchi wa Tabora, ndugu Watanzania nchi yetu inakabiliana na changamoto kubwa nne;

- Uchumi usiozalisha ajira na kutoondoa umasikini

- Huduma duni za jamii hususan Elimu, Afya na Maji

- Rushwa na Ufisadi

- Nyufa katika Taifa kutokana na hisia za udini na ukabila kuanza kushamiri". Mwisho wa kunukuu. 

Leo Mwaka 2017, tukitazama nyuma utaona kuwa hatukuwa na wasiwasi kuhusu Demokrasia na hasa uhuru wa mawazo na Uhuru wa kufikiri tofauti. Hatukuwa na wasiwasi kuhusu Uhuru wa kukosoa Viongozi na kutoa maono mbadala. 

Miaka 2 baadaye huwezi kuandika changamoto za Tanzania bila ya kutaja ufinyu wa demokrasia. Hii ni ishara kuwa tunarudi nyuma. Bahati mbaya ni kwamba baadhi ya Watanzania wanaamini kuwa ili kupata Maendeleo ni lazima kuminya Uhuru wa watu. Tunakosea sana, chama chetu kinaamini kinyume chake.

Demokrasia ni sehemu ya utanzania wetu. Tulianza na demokrasia ya vyama vingi - tukajaribu demokrasia ya chama kimoja na kurejea na demokrasia ya vyama vingi. Hivyo nchi yetu ina uzoefu wa kutosha wa mifumo yote. Historia yetu ni somo tosha la kutufanya tusirudie makosa ya kuamini katika utawala wa kiimla na utawala wa mtu mmoja. 

Wazalendo wenzangu, Katika Ufumaji wa Taifa (StateCraft) - ni muhimu kutambua utofauti wa kihistoria, kinyakati na kimuktadha. Huwezi Leo ukasema kuwa Demokrasia Ndio imeturudisha nyuma na hivyo kutaka kujaribu kuiga mifumo ya nchi nyengine ambazo tunaona zimepiga hatua za kimaendeleo. China, Singapore, Ethiopia na Rwanda kama mfano wa kuigwa? Hapana. Kuna mazuri ya kujifunza na kuchukua lakini sio kila kitu kwani modeli za Maendeleo za nchi hizo zinatokana na historia za maisha yao Kama Taifa na kama watu wanaounda Taifa hilo. 

Nchi zote hizi nilizotaja Kwa mfano zina historia na muktadha tofauti na Tanzania. Mifumo yao imejengwa kwa mujibu wa historia zao, muktadha, na uhalisia wa mataifa yao, kisiasa, kijamii, kiutamaduni na hata kijiografia. Singapore ilijengwa katika muktadha wa vita vya baridi, ambapo mataifa ya kibepari yalilazimika kuibeba kiuchumi ili kuepusha ushawishi wa kiitikadi wa Uchina na Urusi. Ethiopia ilijengwa baada ya kuanguka kwa dola la nchi hiyo na ushindi wa Chama cha Ukombozi cha TPLF, kundi la Meles Zenawi ambaye alipata nafasi ya kuijenga upya nchi hiyo. Rwanda ilijengwa kupya baada ya mauaji ya kimbari yaliyosababisha kuanguka kwa dola na taasisi zote za utawala. Wakaanza upya.

Wazalendo, Tanzania ni tofauti. Tuna historia endelevu. Tuna dola na taasisi za kihistoria ikiwemo taasisi za kidemorasia kama vyama vingi na 'bureaucracy' zilizokomaa. Tuna utamaduni na desturi za utaifa zilizosukwa na kuenziwa kwa weledi mkubwa wa Mwalimu Nyerere na viongozi waliofuata kwa kupitia Azimio la Arusha. 

Tuna historia ya kuthamini misingi ya demokrasia tangia kupata uhuru wetu. Demokrasia imejengeka kwenye mioyo, fikra na matamanio ya wananchi. Hatuwezi kuanza upya na hatuhitaji kufanya hivyo.
Hatua yoyote ya kurejesha nyuma mchakato wa mfumo wa kidemokrasia zitapelekea athari kubwa za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Ni sawasawa na ile hadithi ya jini lililotoka katika kibuyu chake. Unapotaka kulazimisha kulirudisha utaishia kuvunja kibuyu.

Wazalendo, tayari tumeanza kuona madhara hasi ya kuminywa Kwa demokrasia. Kwanza mshikamano uliokuwa umeanza kujengeka ndani ya nchi bila kujali vyama umeanza kumomonyoka. Kamatakamata ya Viongozi wa wananchi badala ya kujenga Taifa inabomoa bomoa nyuzi zinazosuka Utaifa wetu, kujenga chuki na hata kupelekea shughuli za Uchumi kuanza kuporomoka. 

Ukuaji wa sekta ya wananchi wengi, yaani Kilimo cha Mazao ulikuwa 1.4% tu mwaka 2016 kutoka ukuaji wa 2.2% mwaka 2015 na 4% miaka ya kabla ya hapo. Ukichukua kasi ya ukuaji wa idadi ya watu Tanzania ya 2.8% kwa mwaka, maana yake ni kwamba Mwaka 2016 Watanzania tuliongezeka maradufu ya kuongezeka kwa uwezo wetu wa kujilisha. Ina maana mwaka 2016 Watanzania wengi zaidi walidumbukia kwenye umasikini kuliko mwaka 2015. 

Wakati Serikali inaimba Viwanda, mauzo ya bidhaa zitokanazo na Viwanda kwenda nje ya nchi yetu yameshuka sana. Mwaka unaoishia Mei, 2016 Tanzania iliuza nje bidhaa za Viwanda za thamani ya Dola 1.5 bilioni. Mwaka mmoja baadaye yaani mwaka unaoishia Mei, 2017 Tanzania imeuza nje bidhaa za Viwanda za thamani ya Dola 0.8 bilioni tu. Anguko la mauzo Nje la takribani Dola 700 milioni sawa na thamani ya Ndege 23 za Bombadier Q400. 

Uagizaji wa bidhaa za chakula kutoka nje umeongezeka kwa 14% ndani ya mwaka mmoja wa Mei 2016 mpaka Mei 2017 ambapo Tanzania ilitumia Dola 480 milioni kuagiza vyakula kama Sukari, nafaka na mafuta ya Mawese. Tumekuwa tegemezi zaidi, tunauza bidhaa kidogo zaidi nje ya nchi, na tunanunua bidhaa zaidi kutoka nje.

Mauzo ya Nje ya zao la Pamba mwaka 2016 yalikuwa Dola 52 milioni. Mwaka 2017 Mei mauzo yameshuka mpaka Dola 42 milioni. Uagizaji wa bidhaa za kuzalisha bidhaa (capital goods) umeporomoka kwa 25% ndani ya mwaka mmoja kati ya Mei 2016 na Mei 2017. Hali hiyo ya mdororo wa uchumi iko karibia katika sekta zote za uchumi wa nchi yetu.

Takwimu hizi chache zinaonyesha kuwa hali ya nchi yetu sio imara na kuna hatari kwamba Watanzania wengi sana wakadumbukia kwenye umasikini zaidi. 

Mwaka huu ndio tumeshuhudia uminywaji zaidi wa demokrasia na umeendana na kushuka Kwa viashiria vyote vya uchumi. Demokrasia sio adui wa Maendeleo. Demokrasia ni chachu ya Maendeleo. Sisi ACT Wazalendo hatukubaliani na hali hii. Tunaamini kinachopaswa kufanywa ni kusadifu na sio kuikandamiza demokrasia yetu. 

Hilo linapaswa kufanyika katika mfumo unaojenga muafaka wa kitaifa na sio mgawanyiko wa taifa kama inavyoelekea. Na njia thabiti na sahihi ya mchakato huo ni kupata katiba mpya itakayokuwa na ushiriki na ridhaa ya watanzania kwa ujumla wao. Tuthubutu kuenda mbele zaidi na sio kurudi nyuma!

Wazalendo, Yote hayo niliyoyaeleza yanaonyesha Utamaduni wetu wa kisiasa wa kuonana ni Watanzania bila kujali itikadi za vyama vyetu nao umetikiswa, sisi si wamoja tena. Msingi wa utamaduni wetu wa kisiasa hujengwa zaidi kwa mahusiano, matamko na matendo ya viongozi mbalimbali wa nchi. 

Mahusiano, matamko na matendo yetu viongozi katika nyakati hizi yanaashiria mpasuko tu na yanamomonyoa msingi wa amani uliojengwa. Kauli za vitisho na vitendo vya bughdha kwa wote wanaotofautiana mtazamo na watawala ndio vimeshamiri. Yote hayo yameleta athari kwenye uchumi wetu, yamezuia kupatikana kwa sauti mbadala ya kuleta marekebisho ya kisera.

Hali hii inaliathiri Taifa, hatua zifuatazo zichukuliwe kulinda demokrasia yetu na kusukuma mbele Maendeleo yetu:

1. Kwanza ni kwa Viongozi wenzangu, hasa wale wa chama tawala. Ni muhimu Viongozi tuepuke kugawa watu kwa misingi ya vyama vya siasa, makabila, kanda na hata dini. Ni muhimu tuache vitisho kwa wote wanaotumia uhuru wao wa kutoa mawazo mbadala nchini. Ni muhimu tuimarishe uhuru wetu wa kidemokrasia. Tukishindwa kufanya hayo, uhasama utazidi, mpasuko utapanuka, wananchi wetu watapoteza matumaini ya kuwa nchi hii ni moja na kila raia anayo haki (bila kujali tofauti zote za kisiasa, kiuchumi, kidini na kikabila), na mwishowe nchi hii itapasuka vipande vipande, uchumi wetu kudorora zaidi na amani yetu kutoweka.

Vyama vya upinzani vinaongoza Halmashauri zaidi ya 35 nchini, kuzuia mikutano ya hadhara ni uvunjifu wa katiba lakini pia ni kuondoa uwajibishaji kwa tunaoongoza halmashauri hizo kutoka kwa CCM ambao ni wapinzani wetu katika maeneo hayo.

Maeneo kama Kigoma Ujiji tunakoongoza ACT Wazalendo, Arusha Mjini, Mbeya, Iringa nk wananchi wanakosa sauti mbadala, wanakosa uwajibikaji na fursa ya kupatikana kwa mawazo mbadala yanayoweza kuendeleza halmashauri hizo. Hali hiyo ni hivyo hivyo kwenye halmashauri nyengine zinazoongozwa na chama tawala.

2. Kwa wananchi wenzangu, ni muhimu sana kuendelea kupaza sauti kupinga kubanwa kwa Demokrasia, hatupaswi kabisa kukaa kimya, huu ni wajibu wetu wa Kizalendo, hatupaswi kuwaachia nchi wahisani jambo hili. Ndio maana kikao chetu hiki ni muhimu sana, maana kinatupa fursa ya kujadili tusiyokubaliana mtazamo, kujenga muafaka juu ya tunayoridhiana na kushirikiana katika yale tunayokubaliana, ndio ujenzi wa Utaifa, ndio Utanzania. Tunahitaji kuhuisha na kuimarisha utamaduni huu kama tunataka nchi yetu iendelee kuwa ya amani. Tusiache kupaza sauti juu ya Udikteta.

Njia zetu za kupinga udikteta ni lazima zilinde amani yetu, hali hii ya kuwa na viongozi wabaya si jambo jipya duniani, walikuwepo kina Mobutu, Bokassa, Iddi Amin Dada nk, leo hawapo, wakati tukipinga udikteta ni muhimu kuhakikisha amani ya nchi yetu inabaki, Tanzania yetu inabaki.

3. Kwa wazalendo, wanachama wenzangu wa chama cha ACT Wazalendo, tunao wajibu wa kushiriki kujenga Demokrasia ya nchi yetu kwa kupinga Udikteta nchini, lakini wajibu huo ni lazima uambatane na kujihusisha na masuala ya watu. Ni lazima tuendelee kujenga chama chetu hata katika kipindi hiki kigumu, ujenzi huo haupaswi kufanyika mahakamani au jela, ni lazima tukakijenge kwa watu.


Ni lazima tuendelee kuwasemee wananchi, ni lazima tujihusishe na masuala ya watu, ni lazima katika sehemu tunazoongoza tuonyeshe utofauti na wengine, sera nzuri tunazozinadi tuzitekeleze katika maeneo tunayoyaongoza.

Wazalendo, Demokrasia ni hazina na sio laana. Inatupa nafasi ya kujuana na kuthaminiana. Inatupa uwezo wa kutambua mafanikio na mapungufu yetu. Inatoa nafasi kwa mawazo mbadala. Inatuamsha ili tujisahihishe. 

Changamoto tuliyonayo sio mfumo wa kidemokrasia bali ni ukosefu wa wanademokrasia. Sio misingi ya demokrasia bali ni ukosefu wa taasisi imara za kidemokrasia. Sio gharama za mahitaji ya kidemokrasia bali kutambua tija ya siasa za kidemorasia. 

Demokrasia hujenga haki. Haki huzaa amani. Amani huwezesha maendeleo. Tuijenge Demokrasia yetu ili tulete maendeleo ya nchi yetu.

Nataka niwaache na nukuu ya mwanaharakati wa kijamaa wa karne 20,Rosa Luxembourg ambaye alisema 'uhuru kihalisia ni uhuru wa mtu anayefikiri tofauti'. 

Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania

Ahsanteni kwa kunisikiliza

Kabwe Z. Ruyagwa Zitto
Kiongozi wa Chama - ACT Wazalendo Mwanza
Agosti 26, 2017

Thursday, August 24, 2017

Yingluck: Mahakama yatoa kibali waziri mkuu wa zamani Thailand akamatwe

Bangkok, Thailand, 25 August 2017. Mamia ya wafuasi wa Bi Yingluck walifika nje ya majengo ya mahakama ya juu Bangkok 

Mahakama ya Juu nchini Thailand imeahirisha kikao cha kutoa hukumu katika kesi ambapo waziri mkuu wa zamani wa nchi hiyo Yingluck Shinawatra ameshtakiwa makosa ya uhalifu ya kuzembea kazini.
Majaji hao wakiwa mjini Bangkok wametoa kibali cha kukamatwa kwake wakisema hawaamini alivyosema kwamba amekosa kufika mahakamani kwa sababu anaugua.
Mahakama imeahidi kutoa huku tarehe 27 Septemba.

Ijumaa, mawakili wa Bi Yingluck waliomba hukumu icheleweshwe na kuambia mahakama kwamba anaugua ugonjwa wa vertigo na hawangeweza kufika kortini.
Lakini taarifa rasmi ya Mahakama ya Juu imesema waendesha mashtaka "hawaamini mshtakiwa ni mgonjwa kwani hakuna cheti chochote cha matibabu kilichowasilishwa kwa mahakama, na kwamba hali yake ya afya si mbaya mno kiasi kwamba hawezi kufika kortini."
Mahakama imesema itatoa kibali cha kukamatwa kwake kwani anaweza kuikimbia nchi hiyo, kwa mujibu wa shirika la habari la AFP.

Kadhalika, mahakama imetwaa dhamana ya $900,000 (£703,000) ambayo alikuwa ameiweka wakati wa kuanza kwa kesi hiyo.
Bi Yingluck, amekanusha makosa ya kuzembea kazini yanayohusiana na mradi wa mpunga wa gharama ya mabilioni ya dola.
Iwapo atapatikana na hatia, anaweza akafungwa jela na pia kupigwa marufuku kutoshiriki siasa maishani yake yote.

Bi Yingluck, ambaye alikuwa waziri mkuu wa kwanza mwanamke nchini Thailand mwaka 2011, aliondolewa madarakani mwaka 2015.
Kesi dhidi yake iliwasilishwa na serikali inayoungwa mkono na jeshi ambayo ilimuondoa mamlakani.
Lakini bado ni maarufu na anaungwa mkono sana.
Mamia ya wafuasi wake walikusanyika nje ya Mahakama ya Juu mjini Bangkok kabla ya kusomwa kwa hukumu dhidi yake, huku polisi wengi wakishika doria nje ya mahakama hiyo.
Mpango wa Bi Yingluck wa kulipia sehemu ya gharama ya mpunga ulikuwa sehemu ya ahadi zake kuu kwenye kampeni yake ya kutaka kuchaguliwa, na aliuzindua mwaka 2011 muda mfupi baada yake kuingia madarakani.

MPLA yaongoza matokeo ya awali uchaguzi Angola

MPLA imeiongoza angola tokea ilipopata uhuru mwaka 1975MPLA imeiongoza angola tokea ilipopata uhuru mwaka 1975.

Tume ya uchaguzi nchini Angola imesema kwamba matokeo ya awali ya uchaguzi mkuu uliofanyika siku ya Jumatano unaonyesha chama tawala cha MPLA kinaongoza.
Inasema kwamba MPLA imeshinda takriban robo tatu ya kura zote mpaka sasa, huku chama kikuu cha upinzani UNITA kikiwa na asilimia 25.
Waziri wa zamani wa ulinzi Joao Lourenco, anaonekana kuchukua nafasi ya Rais wa muda mrefu Jose Eduardo dos Santos.
Santos ameiongoza Angola kwa karibia miaka 40.

Makuruta washauriwa kutopiga punyeto

Jeshi la taifa hilo limekuwa likishindwa kupata maafisa wapya katika miaka ya hivi karibuni licha ya kuwapongeza wanajeshi wake kuwa wazalendo.

Jeshi la China limewapatia ushauri makurutu wanaotaka kujiunga nalo kuhusu watakavyotakiwa kupita vipimo vya maungo hatua iliosababisha mzaha miongoni mwa watumiaji wa mitandao.
Katika chapisho la mtandao, Jeshi hilo limeshutumu utumiaji wa kupita kiasi wa vinywaji vyenye gesi, uchezaji michezo ya kompyuta na hata kupiga punyeto kama vyanzo vya afya mbaya miongoni mwa vijana .
Imesema kuwa viipimo vya maungo miongoni mwa vijana wengi vimeshuka huku nusu ya wawaniaji wa kazi hizo katika mji mmoja wakifeli.
Jeshi la taifa hilo limekuwa likishindwa kupata maafisa wapya katika miaka ya hivi karibuni licha ya kuwapongeza wanajeshi wake kuwa wazalendo.
Ushauri waliopewa ni:
Ushauri huo ulionekana katika mtandao wa jeshi wa WeChat unaofanana na ule wa WhatsApp mnamo tarehe 19 mwezi Agosti.
Ulionyesha data kutoka mji mmoja wa China ambapo asilimia 56.9 wa vijana waliokuwa wakiwania kazi hizo walifeli kimaungo na kutoa ushauri kwa wanaowania kazi hizo kufuata maagizo 10 muhimu.
  • 1.Kupunguza unywaji wa pombe: Takriban asilimia 25 ya makurutu walifeli vipimo vya damu na mikojo.
  • 2.Tumia muda mchache katika runinga: Asilimia 46 ya makurutu walifeli vipimo vya kuona ambapo jeshi linalaumu utumiaji wa kupitia kiasi wa simu za rununu mbali na vifaa vyengine vya kielektroniki.
  • 3.Fanya mazoezi zaidi: Asilimia 20 ya makurutu walifeli kwa kuwa walikuwa wanene kupitia kiasi.
  • 4.Punguza michezo ya kompyuta pamoja na kupiga punyeto: Asilimia nane walifeli kutokana na uharibifu katika sehemu zao za siri kutokana na kuketi kwa muda mrefu.
  • 5.Jifunze kulala kwa muda: Asilimia 13 ya makurutu walifeli kwa kuwa walikuwa na shinikizo la damu.
  • 6.Usijiweke tatoo
  • 7.Kunywa maji safi: Asilimia 7 walifeli kutokana matatizo ya masikio, pua na koo kutokana na kunywa maji yasio safi.
  • 8.Kufanyiwa matibabu ya magonjwa yanayopitishwa kupitia jeni: Asilimia 3 ya makurutu walifeli kutokana na kutokwa na jasho jingi mwilini .
  • 9.Tafuta tiba ya magonjwa ya kiakili: Asilimia 1.6 walifeli kwa sababu ya maswala ya kiakili hususan shinikizo la kiakili.
  • 10.Kuwa msafi: Asilimia 3.4 ya makurutu walifeli kutokana na magonjwa ya kieneo.
Chapisho hilo lilivutia mzaha huku maelfu ya watu wakiingia katika mtandao wa Weibo kujadili swala hilo.
''Mwaka ujao watataka makurutu kutahiriwa'' , alisema mtumiaji mmoja.
Mtumiaji mwengine alisema ''anashuku kuwa na alama ya kuzaliwa pia ni tatizo kubwa''.
''Kwa nini kuna watu wengi wasio na afya nzuri''?, mtumiaji mmoja aliuliza.
Wengine waliuliza kwa nini watu wanafeli kwa kutoona vizuri.

Tuesday, August 22, 2017

Tetesi za soka Ulaya Jumanne 22.08.2017 na Salim Kikeke

Kylian MbappeKylian Mbappe
Paris Saint- Germain wanakaribia kukamilisha usajili wa mshambuliaji wa Monaco Kylian Mbappe, 18, na Fabinho kwa pauni milioni 200. Mbappe pekee atagharimu pauni milioni 128. PSG pia watamtoa na Lucas Moura katika mkataba huo. (Sky Sport)
Barcelona wamekubali kuwa Liverpool hawatowauzia Philippe Coutinho, 25, mwezi huu. (Mirror)
Kiungo wa Real Madrid Mateo Kovacic, 23, amekubali kwa kauli kujiunga na Liverpool kuziba nafasi ya Philippe Coutinho iwapo ataondoka kwenda Barcelona. (Daily Mirror)
Liverpool bado wanataka kumsajili Virgil van Dijk na watakuwa tayari ikiwa Southampton watabadili msimamo wao kuhusu beki huyo. (Liverpool Echo)Diego Costa
  Diego Costa

Diego Costa, 28, ameambiwa na Atletico Madrid atafute suluhu na Chelsea kwanza kabla ya kununuliwa kwa pauni milioni 25. (Sun)
Kiungo wa Juventus Claudio Marchisio anataka kuondoka Italia na kujiunga na Chelsea. (Corriere della Sera)
Manchester City wanakaribia kukata tamaa ya kumsajili beki wa West Brom Jonny Evans, 29, na badala yake watapanda dau la pauni milioni 20 kumtaka beki wa Middlesbrough Ben Gibson, 24. (Independent)Ross BarkleyRoss Barkley

Tottenham wanajiandaa kupanda dau la pauni milioni 20 kumtaka kiungo wa Everton Ross Barkley, 23, ingawa wanakabiliwa na ushindani kutoka kwa Chelsea pia. (Telegraph)
West Ham tayari wanatafuta kocha wa kuziba nafasi ya Slaven Bilic ambaye amekuwa na mwanzo mbovu wa msimu. (Mirror)
Manchester United wanamtaka kinda wa Fulham Ryan Ssesegnon, 17, ambaye pia anasakwa na Tottenham. (Sky Sports)
Valencia wanakaribia kukamilisha usajili wa mkopo wa kiungo wa Manchester United Andreas Pereira. (Cadena Ser Valencia)
 Julian DraxlerJulian Draxler
Bayern Munich wanafikiria kumsajili mshambuliaji wa Paris Saint-Germain Julian Draxler ambaye hatma yake iko mashakani baada ya kuwasili kwa Neymar. Draxler pia ananyatiwa na Arsenal, Liverpool na Manchester United. (Westdeutsche Allgemeine Zeitung)
Meneja wa Leicester Craig Shakespeare amesema hatma ya Riyad Mahrez, 26, na Danny Drinkwater, 27, pengine haitafahamika mpaka siku za mwisho za dirisha la usajili. (Leicester Mercury)
Beki wa kati wa Southampton ameonekana akifanya mazoezi na kikosi cha chini ya miaka 23 baada ya kuwasilisha maombi ya kuondoka. (Express)
Chelsea hawatopanda dau la kumtaka Virgil van Dijk hadi pale Southampton watakapokuwa tayari ingawa klabu hiyo imesema beki huyo hauzwi. (Telegraph)
Chelsea huenda wakaweza kumsajili Antonio Candreva, 30, kwa sababu Inter Milan inatafuta fedha za kutaka kumsajili Suso, 23, kutoka AC Milan. (Gazzetta dello Sport)Kierran GibbsKierran Gibbs
Galatasaray wanataka kumsajili beki wa Arsenal Kieran Gibbs. (The Times)
Crystal Palace wamepanda dau la pauni milioni 15 kumtaka beki wa Tottenham Kevin Wimmer, ambaye pia anasakwa na West Brom na Stoke. Spurs wanataka pauni milioni 20. (Daily Mail)
Habari zilizothibitishwa tutakujuza mara zitakapothibitishwa. Kwa orodha kamili ya wachezaji waliokamilisha rasmi usajili bofya link hii: http://www.bbc.co.uk/sport/football/transfers
Tetesi nyingine kesho tukijaaliwa. Uwe na wiki njema.