WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Sunday, August 27, 2017

ACT WAZALENDO ILIVYOITINGISHA MWAZA


 Ni katika Mkutano wao mkuu wa Kidemokrasia kukutanisha wanachama, wananchi na viongozi 

 Zitto Kabwe Aunguruma, Azungumzia Uchumi, Kilimo na Demokrasia

Na . Ibrahim Malinda
Zitto Zuberi Kabwe, Kiongozi wa chama cha ACT WAZALENDO juzi aliwaongoza wanachama wa chama hicho katika kuazimisha mkutano wao mkuu wa kidemokrasia wa tatu tangu kuanzishwa kwa chama hicho mkutano uliofanyika mkoani mwanza katika ukumbi wa hotel ya Monarch iliyopo jijini humo.
Ifuatayo ni hotuba iliyosomwa na kiongozi huyo wa chama ambaye pia ni mbunge wa jimbo la kigoma mjini.


Ndugu Watanzania.
Ndugu Wanachama wa Chama cha ACT Wazalendo na washiriki wa Mkutano wetu wa mwaka wa Kidemokrasia hapa Mwanza.

Nawasalimu kwa salaam za kizalendo na kuwakaribisha katika Mkutano wetu wa mwaka 2017. Huu ni Mkutano wetu wa pili wa Kidemokrasia Kwa mujibu wa Katiba ya chama chetu. Agosti mwaka jana tulikuwa Dar es salaam katika Mkutano wa Kwanza wa Kidemokrasia, ambapo tulizungumzia kwa undani juu ya suala la Katiba mpya. 

Mwaka huu mwezi Machi tulikuwa na Mkutano Mkuu wa kidemokrasia maalumu jijini Arusha kuadhimisha miaka 50 ya Azimio la Arusha, kujadili Ujamaa pamoja na umuhimu wa Azimio la Tabora la chama chetu linalohuisha Azimio la Arusha. Leo tupo hapa Mwanza katika Mkutano wa Pili wa Kidemokrasia kuzungumzia umuhimu wa Uhuru wa Fikra, Mawazo na Misingi ya Demokrasia. 

Nina furaha kubwa kwamba pamoja na upya wa chama chetu tumeweza kuendeleza bila kukosa utekelezaji wa Katiba yetu kwamba kila mwaka wanachama wawe na nafasi ya kukutana na viongozi wa chama na wananchi wengine kujadili hali ya nchi yetu kiuchumi, kisiasa na kijamii. Tusiache utamaduni huu kwani ni utamaduni unaoimarisha zaidi Chama na kuweka karibu Viongozi wa Chama na na wanachama; Chama na wananchi; Chama na wadau wake mbalimbali. 

Mkutano huu wa Demokrasia ni utaratibu unaotoa fursa ya moja kwa moja kwa wanachama kutuhoji Viongozi wao, na kushauri juu ya namna njema ya kuendesha siasa zetu. Ni ishara ya kilele cha Demokrasia ya chama chetu. Nawapongeza Sana wanachama na wananchi wote mlioweza kushiriki nasi leo. Nawatakia mjadala wa kina na wenye manufaa Kwa nchi yetu na bara la Afrika. 

Mwaka 2015 wakati wa uzinduzi wa Azimio la Tabora tulizungumza kwenye hotuba ya Tabora kuhusu changamoto ambazo nchi yetu ilikuwa nazo na inawezekana bado inazo . Katika Hotuba ile ambayo imechapishwa kwenye andiko la Azimio la Tabora tulianisha, nanukuu "Wananchi wa Tabora, ndugu Watanzania nchi yetu inakabiliana na changamoto kubwa nne;

- Uchumi usiozalisha ajira na kutoondoa umasikini

- Huduma duni za jamii hususan Elimu, Afya na Maji

- Rushwa na Ufisadi

- Nyufa katika Taifa kutokana na hisia za udini na ukabila kuanza kushamiri". Mwisho wa kunukuu. 

Leo Mwaka 2017, tukitazama nyuma utaona kuwa hatukuwa na wasiwasi kuhusu Demokrasia na hasa uhuru wa mawazo na Uhuru wa kufikiri tofauti. Hatukuwa na wasiwasi kuhusu Uhuru wa kukosoa Viongozi na kutoa maono mbadala. 

Miaka 2 baadaye huwezi kuandika changamoto za Tanzania bila ya kutaja ufinyu wa demokrasia. Hii ni ishara kuwa tunarudi nyuma. Bahati mbaya ni kwamba baadhi ya Watanzania wanaamini kuwa ili kupata Maendeleo ni lazima kuminya Uhuru wa watu. Tunakosea sana, chama chetu kinaamini kinyume chake.

Demokrasia ni sehemu ya utanzania wetu. Tulianza na demokrasia ya vyama vingi - tukajaribu demokrasia ya chama kimoja na kurejea na demokrasia ya vyama vingi. Hivyo nchi yetu ina uzoefu wa kutosha wa mifumo yote. Historia yetu ni somo tosha la kutufanya tusirudie makosa ya kuamini katika utawala wa kiimla na utawala wa mtu mmoja. 

Wazalendo wenzangu, Katika Ufumaji wa Taifa (StateCraft) - ni muhimu kutambua utofauti wa kihistoria, kinyakati na kimuktadha. Huwezi Leo ukasema kuwa Demokrasia Ndio imeturudisha nyuma na hivyo kutaka kujaribu kuiga mifumo ya nchi nyengine ambazo tunaona zimepiga hatua za kimaendeleo. China, Singapore, Ethiopia na Rwanda kama mfano wa kuigwa? Hapana. Kuna mazuri ya kujifunza na kuchukua lakini sio kila kitu kwani modeli za Maendeleo za nchi hizo zinatokana na historia za maisha yao Kama Taifa na kama watu wanaounda Taifa hilo. 

Nchi zote hizi nilizotaja Kwa mfano zina historia na muktadha tofauti na Tanzania. Mifumo yao imejengwa kwa mujibu wa historia zao, muktadha, na uhalisia wa mataifa yao, kisiasa, kijamii, kiutamaduni na hata kijiografia. Singapore ilijengwa katika muktadha wa vita vya baridi, ambapo mataifa ya kibepari yalilazimika kuibeba kiuchumi ili kuepusha ushawishi wa kiitikadi wa Uchina na Urusi. Ethiopia ilijengwa baada ya kuanguka kwa dola la nchi hiyo na ushindi wa Chama cha Ukombozi cha TPLF, kundi la Meles Zenawi ambaye alipata nafasi ya kuijenga upya nchi hiyo. Rwanda ilijengwa kupya baada ya mauaji ya kimbari yaliyosababisha kuanguka kwa dola na taasisi zote za utawala. Wakaanza upya.

Wazalendo, Tanzania ni tofauti. Tuna historia endelevu. Tuna dola na taasisi za kihistoria ikiwemo taasisi za kidemorasia kama vyama vingi na 'bureaucracy' zilizokomaa. Tuna utamaduni na desturi za utaifa zilizosukwa na kuenziwa kwa weledi mkubwa wa Mwalimu Nyerere na viongozi waliofuata kwa kupitia Azimio la Arusha. 

Tuna historia ya kuthamini misingi ya demokrasia tangia kupata uhuru wetu. Demokrasia imejengeka kwenye mioyo, fikra na matamanio ya wananchi. Hatuwezi kuanza upya na hatuhitaji kufanya hivyo.
Hatua yoyote ya kurejesha nyuma mchakato wa mfumo wa kidemokrasia zitapelekea athari kubwa za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Ni sawasawa na ile hadithi ya jini lililotoka katika kibuyu chake. Unapotaka kulazimisha kulirudisha utaishia kuvunja kibuyu.

Wazalendo, tayari tumeanza kuona madhara hasi ya kuminywa Kwa demokrasia. Kwanza mshikamano uliokuwa umeanza kujengeka ndani ya nchi bila kujali vyama umeanza kumomonyoka. Kamatakamata ya Viongozi wa wananchi badala ya kujenga Taifa inabomoa bomoa nyuzi zinazosuka Utaifa wetu, kujenga chuki na hata kupelekea shughuli za Uchumi kuanza kuporomoka. 

Ukuaji wa sekta ya wananchi wengi, yaani Kilimo cha Mazao ulikuwa 1.4% tu mwaka 2016 kutoka ukuaji wa 2.2% mwaka 2015 na 4% miaka ya kabla ya hapo. Ukichukua kasi ya ukuaji wa idadi ya watu Tanzania ya 2.8% kwa mwaka, maana yake ni kwamba Mwaka 2016 Watanzania tuliongezeka maradufu ya kuongezeka kwa uwezo wetu wa kujilisha. Ina maana mwaka 2016 Watanzania wengi zaidi walidumbukia kwenye umasikini kuliko mwaka 2015. 

Wakati Serikali inaimba Viwanda, mauzo ya bidhaa zitokanazo na Viwanda kwenda nje ya nchi yetu yameshuka sana. Mwaka unaoishia Mei, 2016 Tanzania iliuza nje bidhaa za Viwanda za thamani ya Dola 1.5 bilioni. Mwaka mmoja baadaye yaani mwaka unaoishia Mei, 2017 Tanzania imeuza nje bidhaa za Viwanda za thamani ya Dola 0.8 bilioni tu. Anguko la mauzo Nje la takribani Dola 700 milioni sawa na thamani ya Ndege 23 za Bombadier Q400. 

Uagizaji wa bidhaa za chakula kutoka nje umeongezeka kwa 14% ndani ya mwaka mmoja wa Mei 2016 mpaka Mei 2017 ambapo Tanzania ilitumia Dola 480 milioni kuagiza vyakula kama Sukari, nafaka na mafuta ya Mawese. Tumekuwa tegemezi zaidi, tunauza bidhaa kidogo zaidi nje ya nchi, na tunanunua bidhaa zaidi kutoka nje.

Mauzo ya Nje ya zao la Pamba mwaka 2016 yalikuwa Dola 52 milioni. Mwaka 2017 Mei mauzo yameshuka mpaka Dola 42 milioni. Uagizaji wa bidhaa za kuzalisha bidhaa (capital goods) umeporomoka kwa 25% ndani ya mwaka mmoja kati ya Mei 2016 na Mei 2017. Hali hiyo ya mdororo wa uchumi iko karibia katika sekta zote za uchumi wa nchi yetu.

Takwimu hizi chache zinaonyesha kuwa hali ya nchi yetu sio imara na kuna hatari kwamba Watanzania wengi sana wakadumbukia kwenye umasikini zaidi. 

Mwaka huu ndio tumeshuhudia uminywaji zaidi wa demokrasia na umeendana na kushuka Kwa viashiria vyote vya uchumi. Demokrasia sio adui wa Maendeleo. Demokrasia ni chachu ya Maendeleo. Sisi ACT Wazalendo hatukubaliani na hali hii. Tunaamini kinachopaswa kufanywa ni kusadifu na sio kuikandamiza demokrasia yetu. 

Hilo linapaswa kufanyika katika mfumo unaojenga muafaka wa kitaifa na sio mgawanyiko wa taifa kama inavyoelekea. Na njia thabiti na sahihi ya mchakato huo ni kupata katiba mpya itakayokuwa na ushiriki na ridhaa ya watanzania kwa ujumla wao. Tuthubutu kuenda mbele zaidi na sio kurudi nyuma!

Wazalendo, Yote hayo niliyoyaeleza yanaonyesha Utamaduni wetu wa kisiasa wa kuonana ni Watanzania bila kujali itikadi za vyama vyetu nao umetikiswa, sisi si wamoja tena. Msingi wa utamaduni wetu wa kisiasa hujengwa zaidi kwa mahusiano, matamko na matendo ya viongozi mbalimbali wa nchi. 

Mahusiano, matamko na matendo yetu viongozi katika nyakati hizi yanaashiria mpasuko tu na yanamomonyoa msingi wa amani uliojengwa. Kauli za vitisho na vitendo vya bughdha kwa wote wanaotofautiana mtazamo na watawala ndio vimeshamiri. Yote hayo yameleta athari kwenye uchumi wetu, yamezuia kupatikana kwa sauti mbadala ya kuleta marekebisho ya kisera.

Hali hii inaliathiri Taifa, hatua zifuatazo zichukuliwe kulinda demokrasia yetu na kusukuma mbele Maendeleo yetu:

1. Kwanza ni kwa Viongozi wenzangu, hasa wale wa chama tawala. Ni muhimu Viongozi tuepuke kugawa watu kwa misingi ya vyama vya siasa, makabila, kanda na hata dini. Ni muhimu tuache vitisho kwa wote wanaotumia uhuru wao wa kutoa mawazo mbadala nchini. Ni muhimu tuimarishe uhuru wetu wa kidemokrasia. Tukishindwa kufanya hayo, uhasama utazidi, mpasuko utapanuka, wananchi wetu watapoteza matumaini ya kuwa nchi hii ni moja na kila raia anayo haki (bila kujali tofauti zote za kisiasa, kiuchumi, kidini na kikabila), na mwishowe nchi hii itapasuka vipande vipande, uchumi wetu kudorora zaidi na amani yetu kutoweka.

Vyama vya upinzani vinaongoza Halmashauri zaidi ya 35 nchini, kuzuia mikutano ya hadhara ni uvunjifu wa katiba lakini pia ni kuondoa uwajibishaji kwa tunaoongoza halmashauri hizo kutoka kwa CCM ambao ni wapinzani wetu katika maeneo hayo.

Maeneo kama Kigoma Ujiji tunakoongoza ACT Wazalendo, Arusha Mjini, Mbeya, Iringa nk wananchi wanakosa sauti mbadala, wanakosa uwajibikaji na fursa ya kupatikana kwa mawazo mbadala yanayoweza kuendeleza halmashauri hizo. Hali hiyo ni hivyo hivyo kwenye halmashauri nyengine zinazoongozwa na chama tawala.

2. Kwa wananchi wenzangu, ni muhimu sana kuendelea kupaza sauti kupinga kubanwa kwa Demokrasia, hatupaswi kabisa kukaa kimya, huu ni wajibu wetu wa Kizalendo, hatupaswi kuwaachia nchi wahisani jambo hili. Ndio maana kikao chetu hiki ni muhimu sana, maana kinatupa fursa ya kujadili tusiyokubaliana mtazamo, kujenga muafaka juu ya tunayoridhiana na kushirikiana katika yale tunayokubaliana, ndio ujenzi wa Utaifa, ndio Utanzania. Tunahitaji kuhuisha na kuimarisha utamaduni huu kama tunataka nchi yetu iendelee kuwa ya amani. Tusiache kupaza sauti juu ya Udikteta.

Njia zetu za kupinga udikteta ni lazima zilinde amani yetu, hali hii ya kuwa na viongozi wabaya si jambo jipya duniani, walikuwepo kina Mobutu, Bokassa, Iddi Amin Dada nk, leo hawapo, wakati tukipinga udikteta ni muhimu kuhakikisha amani ya nchi yetu inabaki, Tanzania yetu inabaki.

3. Kwa wazalendo, wanachama wenzangu wa chama cha ACT Wazalendo, tunao wajibu wa kushiriki kujenga Demokrasia ya nchi yetu kwa kupinga Udikteta nchini, lakini wajibu huo ni lazima uambatane na kujihusisha na masuala ya watu. Ni lazima tuendelee kujenga chama chetu hata katika kipindi hiki kigumu, ujenzi huo haupaswi kufanyika mahakamani au jela, ni lazima tukakijenge kwa watu.


Ni lazima tuendelee kuwasemee wananchi, ni lazima tujihusishe na masuala ya watu, ni lazima katika sehemu tunazoongoza tuonyeshe utofauti na wengine, sera nzuri tunazozinadi tuzitekeleze katika maeneo tunayoyaongoza.

Wazalendo, Demokrasia ni hazina na sio laana. Inatupa nafasi ya kujuana na kuthaminiana. Inatupa uwezo wa kutambua mafanikio na mapungufu yetu. Inatoa nafasi kwa mawazo mbadala. Inatuamsha ili tujisahihishe. 

Changamoto tuliyonayo sio mfumo wa kidemokrasia bali ni ukosefu wa wanademokrasia. Sio misingi ya demokrasia bali ni ukosefu wa taasisi imara za kidemokrasia. Sio gharama za mahitaji ya kidemokrasia bali kutambua tija ya siasa za kidemorasia. 

Demokrasia hujenga haki. Haki huzaa amani. Amani huwezesha maendeleo. Tuijenge Demokrasia yetu ili tulete maendeleo ya nchi yetu.

Nataka niwaache na nukuu ya mwanaharakati wa kijamaa wa karne 20,Rosa Luxembourg ambaye alisema 'uhuru kihalisia ni uhuru wa mtu anayefikiri tofauti'. 

Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania

Ahsanteni kwa kunisikiliza

Kabwe Z. Ruyagwa Zitto
Kiongozi wa Chama - ACT Wazalendo Mwanza
Agosti 26, 2017

No comments:

Post a Comment