WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Sunday, August 6, 2017

Kitanzi cha Maalim Seif ni Katiba ya CUF




Ibara ya 117 ya katiba ya CUF ndio mwiba kwake,

Inaelekeza kiongozi anayetaka kujiuzulu lazima akubaliwe na mamlaka iliyomchagua

Yeye na Mtatiro walimpuuza Lipumba, Sasa wanahaha kujinusuru

Mipango kumuangushia lawama msajili wa vyama ,serikali yazidi kugognga mwamba

Kila mahali waambiwa fuateni katiba yenu.

Na Ibrahim Malinda.


KUKWAMA  kwa majaribio kadhaa ya Katibu Mkuu wa chama cha wananchi( CUF) Maalim Seif Sharif Hamad dhidi ya Mwenyekiti wake Profesa Ibrahim Lipumba na viongozi wake waandamizi aliowateua na wengine kuteuliwa na vyombo vya maamuzi vya chama hicho kunatokana na katiba ya chama hicho, imezidi kubainika.

Hivi karibuni Katibu Mkuu wa Chama hicho, Maalim Seif alipata pigo baada ya kukwama kwa  jaribio lake la kuwavua uanachama wanachama kadhaa wa chama hicho akiwemo Magdalena Sakaya ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa CUF Bara na Kaimu Katibu Mkuu wa chama hicho Taifa ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Kaliua, Mkoani Tabora sambamba na Maftah Nachuma ambaye ni mbunge wa Mtwara Mjini.

Sambamba na jaribio hilo kukwama, wiki chache zilizopita Wakala wa Usajili, Ufilisi na Uthamini(RITA) iliridhia usajili wa wajumbe wapya wa bodi ya wadhamini baada ya kuisha kwa muda wa bodi ya awali ya udhamini wa chama hicho.

Jambo hilo linathibitisha kumuondoa Maalim Seif katika nafasi ya kushinda imani ya wananchama wa CUF baada ya kuenea kwa tetesi kwamba bodi mpya ya wadhamini imeunda na wanachama wanaomuunga mkono Mwenyekiti wa Chama hicho, Profesa Lipumba.

Kitendo cha kutambuliwa kwa bodi mpya ya wadhamini wa CUF, kinatoa taswira kuwa kuna uwezekano wa kufutwa kwa mashtaka yote yaliyofunguliwa na bodi ya awali ya udhamini, bodi ambayo kwa mujibu wa katiba ya chama hicho, ndio imepewa mamlaka ya kushtaki na kushtakiwa kwa niaba ya chama cha CUF.

Aidha maung’uniko ya muda mrefu ya katibu mkuu huyo wa chama hicho kuwa kurudi kwenye kiti kwa mwenyekiti wake Lipumba kunatokana na kubebwa na ofisi ya msajili wa vyama vya siasa nchini inayoongozwa na jaji Fransis Mutungi yameonekana kukosa mashiko.

Hali hiyo, inatokana na Lipumba baada ya kujua kwamba katiba ya chama hicho inamruhusu kutengua uamuzi wake kutokana na kutokukubaliwa kwa ombi lake na mamlaka iliyomchagua.
Taarifa zaidi zinasema kwamba kuzembea kwa katibu mkuu huyo kuchukua uamuzi wa kuitisha mkutano mkuu wa chama hicho haraka mara tu baada ya kupokea barua ya Lipumba ya kujiuzulu  ambapo mkutano huo ungepiga kura ya siri ya kuridhia ombi hilo na hatimaye Lipumba kuwa ameondoka rasmi kwa kufuata matakwa ya katiba ndiko kumesababisha mtanziko unaendelea hivi sasa.

‘’Katiba ilimtaka katibu mkuu kuitisha mkutano mkuu maalum kwa ajili ya kujadili na kupiga kura juu ya barua ya Profesa lakini Maalim hakuitisha, hiyo hata ule mkutano wa Agosti 21 pale ubungo plaza haukuwa na lengo la kujadili barua ya Profesa bali ni kuchagua tu Mwenyekiti ambapo kina Taslima walikuwa wanagombea, lakini tulipokataa kwa nguvu ndio ikachomekwa hiyo agenda na hata hivyo hatukufikia hatua ya kupiga kura’’. Anasema mjumbe mmoja wa mkutano mkuu wa chama hicho kutokea viwani Zanzibar tunayemuhifadhi jina lake kwa sasa.

Kwa kifupi  Ibara ya 117(2) ya katiba ya CUF inataka ili kiongozi ahesabike amejiuzulu ni lazima mamlaka iliyomchagua ikubali ombi lake, ambapo kwa Profesa Lipumba mamlaka hiyo ni Mkutano mkuu wa chama hicho ambao haujaridhia ombi hilo . Hata hivyo Maalim Seif na timu yake wanaukwepa ukweli huo wa katiba yao na kueneza propaganda dhidi ya Msajili na Serikali.

Ibara hiyo ya 117 kifungu kidogo cha (2) inasomeka kama ifuatavyo  ‘’Kiongozi atajiuzulu kwa kuandika barua na kuweka saini yake kwa katibu wa mamlaka iliyomchagua au kumteua na kiongozi  huyo atahesabiwa kuwa amejiuzulu ikifika tarehe aliyoiainisha katika barua yake kuwa atajiuzulu pindipo akikubaliwa na mamlaka iliyomchagua au iliyomteua, au kama hakuainisha tarehe ya kujiuzulu kwake basi atahesabiwa amejiuzulu mara baada ya katibu wa mamlaka iliyomteua au kumchagua kupokea barua hiyo na mamlaka iliyomchagua au kumteua kukubali ’’.

Hivi karibuni gazeti hili liliripoti kuwa hali ya mambo inazidi kwenda kombo kwa upande wa Maalim Seif katika mgogoro wa kiuongozi unaoendelea baina yake na mwenyekiti wa Taifa wa Lipumba.

Kitendo cha Mwenyekiti wa Chama hicho, Profesa Lipumba kuwavua uanachama wabunge nane na madiwani wawili wa viti maalum kitendo kilichoonyesha kufuata taratibu zote za kisheria na katiba ya ndani ya chama hicho na hatimaye kubarikiwa na ofisi ya Bunge, Tume ya taifa ya Uchaguzi na msajili wa vyama vya siasa.

Taarifa zaidi inaelezwa kinaelezwa kumpagawisha Katibu Mkuu huyo na timu yake kiasi cha kuamua na yeye kuwavua uanachama wanachama wengine kadhaa akiwemo mbunge na Naibu Katibu Mkuu anayekaimu majukumu ya Katibu Mkuu wa chama hicho kwa sasa kutokana na kutokufika ofisini kwa Maalim Seif tangu mwezi Septemba, 2016.

Mmoja wa wanaharakati wa siasa nchini, Joseph Zabron, alisema huu ndio wakati wa Maalim Seif kukaa mezani na Profesa Lipumba kuyamaliza mambo yote kwa kuwa chama imara ni maelewano na si kuanza kutoa shutuma kwa vyombo vya dola.

“Hili suala ukilitizama kwa umakini si Msajili wa Vyama, Bunge wala Tume au Mahakama unaweza ukasema inaingilia CUF zaidi ya Katiba yao wenyewe na ndio maana wao wenyewe wamekwenda mahakamani kukatia rufaa maamuzi ya msajili, lakini maamuzi halali hayakatiwi rufaa,’’alisema.

Kadhalika, wakati hayo yanaendelea hivi karibuni Mwenyekiti wa Chama hicho alifanikiwa kusajili upya bodi ya wadhamini wa chama hicho baada ya ile ya awali kumaliza muda wake wa mujibu wa sheria jambo ambalo limezidisha pigo kwa timu ya maalim seif kwa sababu bodi ya wadhamini ya chama chochote cha siasa huwa moja tu inayosajiliwa na RITA na kwa mujibu wa katiba ya CUF bodi hiyo ndio mamlaka pekee inayoruhusiwa kufanya usimamizi wa jumla wa chama hicho ikiwemo kushtaki na kushtakiwa jambo linalohatarisha uwepo na uhalali wa kesi zilizofunguliwa na bodi ya awali dhidi ya Msajili wa vyama na Lipumba juu ya masuala kadhaa.

Aidha, kukwama huko kwa maalim Seif katika kile anachokiita mapambano ya kukinusuru chama hicho, kunamfanya sasa abadili mawazo na kujiandaa kuhamia chama kingine kikubwa cha upinzani hapa nchini chenye ngome yake kuu Tanzania bara.

Taarifa zaidi zinaonyesha kwamba mpaka sasa maalim na watu wake wameshakubali kuwa kisheria hawawezi kumshinda Prof. Lipumba na kwamba wamebakiwa na njia mbili pekee ama wahame kuhamia chama hicho kikubwa cha upinzani Tanzania bara ama waanzishe chama chao wenyewe kipya.

Mjadala unaoendelea hivi sasa baina ya wadau muhimu wa timu ya maalim Seif ni kwamba iwapo uamuzi utakuwa ni kuwa wanahama, je watahama na vyeo vyao walivyokuwa navyo wakiwa CUF kama hicho cha Katibu mkuu na vya baadhi ya vya wakurugenzi au watahamia na kuwa wanachama wa kawaida jambo ambalo wanahisi litawapunguzia nguvu ya kufanikisha agenda yao ya kuendelea kudai maslahi yao ya kisiasa yanayotokana nauchaguzi mkuu uliopita.

Taarifa hizo pia zinaeleza kuwa mpaka sasa majadiliano ya kina ya namna gani Maalim na timu yake watahamia chama hicho yameshaanza na yanaratibiwa vizuri na wanasiasa kadhaa mashughuli hapa nchini wakishirikiana na baadhi ya wafanyabiashara wenye vinasaba na chama hicho.

Ikiwa mwanasiasa huyo atahama chama hicho na kujiunga chama kingine kama njia ya kufikia lengo lake la kisiasa, kitakuwa ni kielelezo mahsusi cha kudhibitiwa na Prof. Lipumba katika kuijua na kuifahamu katiba ya chama hicho na pia ndio utakuwa mwisho wa ushirikiano wa Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA.

Alipotafutwa na gazeti hili msajili wa vyama vya siasa Jaji Fransis Mutungi, ameendelea kusisitiza kwamba ofisi yake itaendelea kufanya kazi za kuvisimamia vyama vyote vya siasa vilivyopo hapa nchini kama sheria iliyoviasisi inavyosema na kuongeza kuwa kinachoendelea ndani ya Cuf ni matokeo ya utekelezaji wa katiba ya chama hicho ambacho wameitunga wenyewe.

‘’mimi ofisini kwangu ninasajili vyama baada ya kuzipitia katiba zao na kujiridhisha kuwa hazikiuki masharti ya sheria za nchi, nikizipokea na kujiridhisha siongezi wala kupunguza kitu chochote zaidi ya kuzisajili, na kama ujuavyo katiba ikishapitishwa kinachofuata ni kutekelezwa tu’’. Alisema Msajili Mutungi

‘’kwa hiyo Lugha nyepesi kabisa kuitumia ni kwamba mchawi wa Cuf si Mutungi wala nani, Mchawi wa Cuf ni katiba yao wenyewe, waifate katiba yao inavyoelekeza nina imani hakuna malalamiko yatakayotokea, lakini kama wataendelea kufanya mambo kwa hisia na utashi binafsi, basi haya wataendelea kulalamikiana daima’’. Aliongeza mtaalamu huyo wa maswala ya sheria.

No comments:

Post a Comment