WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Monday, November 6, 2017

MAPINDUZI SEKTA YA MAJI


Na. Ibrahim Malinda 

Wakati jana Rais wa Jamhuro ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli ametimiza miaka miwili tangu aapishwe kuwa Rais wan chi, sekta ya maji imekuwa ni miongoni mwa sekta zilizofanikiwa kwa kiasi kikubwa sana na kupigiwa mfano.

Uzinduzi wa miradi mikubwa ya maji kama ule wa ruvu chini, mradi wa kutoa maji ziwa Victoria na kuyapeleka mikoa ya jirani, mradi wa maji kigoma, mradi wa misungwi , mradi mkubwa wa maji wa lindi na mingineyo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya serikali hii ya awamu ya tano.

Jiji la Dar es salaam kwa sasa sehemu kubwa yake imekuwa ikipata huduma ya maji ya bomba hata kwenye maeneo yaliyosemwa kuwa korofi na malalamiko ya upatikanaji wa maji kuwa makubwa lakini sasa imekuwa tofauti.

‘’kwa kweli sasa hivi hawa DAWASCO waje watengeneze mabomba tu ili maji yasiendelee kumwagika maana maji yamekuwa mengi mno’’. Anasema mkazi wa tabata Mariam Abdalaah
‘’huku tabata hapo nyuma ilikuwa ukitaka kuhamia unaambiwa kuhusu shida ya maji, na mara chache yalikuwa yanatoka kwa kuvizia pengine hata mara moja kwa mwezi, lakini kwa sasa tunajionea wenyewe yanavyotiririka. Tunawapongeza sana kwa hatua hii muhimu, maji ni uhai bwana’’. Aliongeza

Aidha, utaratibu wa serikali kuwagia maji wananchi kwa kulipa kidogo kidogo (yaani mkopo) kumeonyesha uwepo wa mapinduzi makubwa na utayari wa kipekee wa serikali kuhakikisha huduma hii muhimu inawafikia wananchi wote bila kujali vipato vyao.
Mwanabaraka Habibu ni miongoni mwa wanufaika wa utaratibu huu na anasema umemfanya ajisikie mwenye furaha sana kwa kuwa na uhakika wa maji safi na salama
‘’hata sijui niseme nini, yaani nimefungiwa bomba hilo hapo na nalipa taratibu taratibu mpaka deni liishe, mambo ya kudamka alfajir kuwahi foleni tumesha sahau kwa sasa. Mungu atupe nini tena?’’ alinukuliwa
Hivi karibuni katibu mkuu wa wizara ya maji na numwagiliaji Profesa Kitila Mkumbo ameandika makala maalum inayofafanua na kuelekeza masuala mbalimbali kuhusiana na mafanikio, mipango na matarajio ya wizara hiyo katika kuhakikisha watanzania wanapata maji safi na salama.

Miaka Miwili ya JPM:
Kazi kubwa imefanyika na inaendelea kufanyika katika sekta ya maji
Kitila Mkumbo
Wataalam maendeleo duniani wanakubaliana kwamba maji ndicho kiungo na kichocheo kikubwa cha maendeleo katika dunia ya leo. Bila maji hakuna maendeleo. Bila maji hakuna maisha. Ndiyo maana hata wataalam wa anga wanatumia uwepo wa maji kama mojawapo ya vielelezo vya uwezekano wa kuwepo maisha katika sayari zingine. Maji ni bidhaa ya pekee duniani yenye uhitaji kwa wote kwa wakati wote. Upekee wa maji unatokana na ukweli kwamba bidhaa hii haina mbadala. Ukikosa kuni za kupikia utatumia majiko ya umeme, mkaa, gesi, mafuta ya taa, au umemejua. Ukikosa umeme utatumia mwanga wa jua; utawasha koroboi na unaweza kuamua kulala gizani.
 Upo uhusiano mkubwa baina ya ukosekanaji wa maji na kiwango cha maendeleo. Ripoti mbalimbali zimeonyesha kuwa moja ya kiashiria cha nchi zilizo nyuma kimaendeleo ni tatizo la upatikanaji wa maji kwa watu wake. Ni kwa sababu hii Rais John Pombe Magufuli alitamka wazi wakati akifungua rasmi Bunge jipya la Jamhuri wa Muunghano wa Tanzania kuwa Tunataka tuwatue akina mama ndoo kichwani. Tunatambua umaskini hauwezi kuondoka nchini kama wananchi hawapati maji safi na salama”.

Lakini kama hakuna maji utaoga nini? Utapikia nini ili chakula kiive? Utafulia nini nguo chafu? Utakunywa nini ili uweze kukata kiu ya maji mwilini? Kama hakuna maji, pasina shaka kabisa, ndoto ya nchi ya viwanda itayeyuka! Ujenzi utasimama! Hoteli na nyumba za kulala wageni zitafungwa! Wafanyakazi hawataweza kwenda kazini, wanafunzi hawatakwenda shuleni! Hakuna mbadala wa maji!
Ni kwa sababu ya upekee wa maji, nchi zote duniani huiweka sekta ya maji kama kipaumbele mojawapo kikubwa katika mipango ya maendeleo. Hivyo ndiyo ilivyo pia kwa Tanzania ambapo sekta ya maji ni moja ya vipaumbele kumi (10) vya kitaifa katika mpango wa miaka mitano wa maendeleo.
Mwezi huu wa Novemba 2017, Rais Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ametimiza miaka miwili (2) tangu alipoapa na kukubali kuongoza Tanzania. Katika makala hii ninaainisha mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika miaka miwili ya uongozi wa Rais Magufuli katika sekta ya maji.
Maendeleo katika sekta ya maji hupimwa kwa vigezo vikubwa vitatu. Mosi, tunaangalia uwepo, utunzaji, uendelezaji na ukuzaji wa rasilimali ya maji. Pili, tunaangalia uwezo na kasi ya usambazaji wa raslimali ya maji kwa matumizi mbalimbali, kama vile matumzi ya nyumbani, viwandani, mashambani na kwa ajili ya kutunza mazingira. Tatu, tunaangalia uwezo na kasi ya uondoaji wa majitaka, kwa kuzingatia kuwa takribani asilimia 80 ya maji yanayotumika majumbani hugeuka kuwa majitaka yanayostahili kuondolewa na kuhifadhiwa katika namna ambayo haileti madhara ya kiafya kwa binadamu na mazingira. https://pbs.twimg.com/profile_images/848146090545344517/zZthBN-V.jpg
Prof. Kitila Mkumbo, Katibu mkuu wizara ya maji na umwagiliaji.
Kwa lengo la makala hii, nitajikita katika mafanikio yaliyopatikana na changamoto zilizojitokeza katika usambazaji wa maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu, yaani usambazaji wa maji safi na salama ya kunywa. Hata hivyo, itoshe tu kusema kwa sasa kuwa, tofauti na imani kuwa tuna maji mengi chini na juu ya ardhi, ukweli ni kuwa katika miaka 50 iliyopita, raslimali hii imekuwa ikipungua ukilinganisha na kasi ya ongezeko la idadi ya watu.
Kwa mfano, wakati mwaka 1962 Tanzania ilikuwa na wastani wa kiasi cha maji mita za ujazo 7,862 (sawa na mapipa 39,310 ) kwa mtu mmoja kwa mwaka, kiwango hiki kimeshuka hadi mita za ujazo 1,621 (sawa na mapipa 8105)  ilipofika mwaka 2014. Kiwango hiki ni kidogo na kinaiweka Tanzania kuwa moja ya nchi inayokabiliwa na uhaba wa maji duniani. Upungufu huu umetokana na sababu mbalimbali, nyingi zikiwa ni matokeo ya shughuli zetu wenyewe kama vile kuharibu vyanzo vya maji, kukata misitu na teknolojia ndogo ya kuhifadhi maji. Sababu zingine ni zile ambazo kwa kiasi kikubwa kipo nje ya uwezo wetu kama vile mabadiliko ya tabianchi. Hii inamaanisha kuwa tuna kazi kubwa kama taifa ya kufanya katika kuhuisha, kulinda na kuendeleza vyanzo mbalimbali za maji. Ni kwa sababu hii, serikali, kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo, inatekeleza mipango mbalimbali ya kulinda na kuendeleza vyanzo vya maji.
Njia moja ya kuboresha upatikanaji wa maji hata machache yaliyopo ni kuimarisha mfumo wa usambazaji ili maji yaliyopo yaweze kukidhi haja ya matumizi yetu. Mfumo wa usambazaji wa maji katika nchi yetu umegawanywa katika makundi makubwa manne, ambayo ni Dar es Salaam, miji mikuu ya mikoa, miji midogo na makao makuu ya wilaya na vijijini. Katika sehemu zinazofuata za makala hii ninaainisha hatua mbalimbali ambazo serikali imechukua na mafanikio yaliyopatikana katika kusambaza maji kwa maeneo haya.

Usambazaji wa maji Dar es Salaam
Hatua nne muhimu zimechukuliwa na zinaendelea kuchukuliwa katika kupanua miundo mbinu ya usambazaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam pamoja na maeneo ya Kibaha na Bagamoyo. Hatua ya kwanza ilikuwa ni ukarabati na upanuzi wa mitambo ya kuzalisha maji katika Mto Ruvu. Mto huu ndio chanzo kikuu cha maji kwa Jiji la Dar es Salaam na miji ya Kibaha na Bagamoyo ukichangia kwa asilimia 98. Katika miaka ya mwanzo ya 1990 kuelekea miaka ya 2000 uwezo wa mitambo hii kuzalisha maji ulipungua sana ukilinganisha na mahitaji. Mitambo hii ilikuwa inazalisha lita milioni 300 (mapipa milioni 1.5) kwa siku wakati mahitaji halisi yalikuwa ni lita milioni zaidi ya 500 (mapipa milioni 2.5).
Kwa kutambua hili, serikali, kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo, iliwekeza shilingi bilioni 443 kwa ajili ya kupanua mitambo ya Ruvu Juu na Ruvu Chini. Kazi imekamilika mapema mwaka huu na mitambo ya Ruvu Juu ilizinduliwa rasmi na Mhe Rais Dkt John Magufuli mwezi Juni 2017. Kufuatia hatua hii, uzalishaji wa maji wa mitambo hii sasa umeongezeka hadi kufukia lita milioni 502 kwa siku wakati mahitaji halisi ni lita milioni 544.
Hatua ya pili ni uchimbaji wa visima 20 katika maeneo ya Kimbiji na Mpera kwa gharama ya shilingi bilioni 18. Visima hivi kwa pamoja vitakuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 260 kwa siku, na hivyo kufikisha jumla ya lita milioni 760 kwa siku kwa Jiji la Dar es Salaam. Uzalishaji huu utatosheleza mahitaji ya Jiji la Dar es Salaam na maeneo ya Kibaha na Bagamoyo angalau hadi mwaka 2030. Uchimbaji wa visima 19 ulikamilika Oktoba 2017. Serikali tayari imeanza mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kuweka miundombinu ya usambazaji. Maeneo yatakayonufaika na mradi huu ni pamoja na Kigamboni, Keko, Chamazi, Mbagala, Kongowe, Ukonga, Gongolamboto, Pugu, Chanika, n.k. Zinahitajika jumla ya shilingi bilioni 465 kwa ajili ya kuwekeza katika miundombinu ya usambazaji katika maeneo haya.
Hatua ya tatu ni kuwekeza katika miundombinu ya kusambaza maji kutoka Ruvu Juu na Ruvu Chini. Miundombinu hii ni pamoja na usimikaji wa mabomba na ujenzi wa matanki makubwa ya kuhifadhi maji katika maeneo ya Kimara, Mbezi na Makongo. Miundombinu hii itagharimu jumla ya shilingi biloni 290 na inatarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa mwaka huu. Kukamilika kwa mradi huu kutamaliza kabisa tatizo la upatikanaji wa maji katika maeneo ya Mbezi Beach, Kinyerezi, Kimara, Kiluvya, Tegeta, Bagamoyo, Changanyikeni, Wazo, Bunju, Salasala, Goba, n.k. Baadhi ya wakazi wa maeneo haya tayari wameanza kupata maji ya uhakika kwa zaidi ya masaa 20 kwa siku na hali hii itaendelea kuboreka na kuimarika kabisa ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Hatua ya nne ni ujenzi wa Bwawa la Kidunda lililopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro. Katika miaka ya hivi karibuni Mto Ruvu umeanza kupungua maji hasa nyakati za kiangazi. Hali hii inatishia uhakika wa maji katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo mengine yanayohudumiwa na mitambo ya Ruvu Juu na Chini. Hali inatarajiwa kuwa mbaya zaidi kutokana na mabadiliko ya tabianchi na kasi kubwa ya ongezeko la watu katika Jiji la Dar es Salaam. Kwa kutambua hili, serikali imewekeza katika mradi wa ujenzi wa Bwawa la Kidunda kwa lengo la kuwa na chanzo cha uhakika wa maji kutiririka katika Mto Ruvu na kuondoa kabisa tatizo la kupungua kwa uwezo wa uzalishaji kwa kutumia Mto Ruvu. Gharama za mradi huu ni takribani shilingi bilioni 483. Hadi sasa, kati ya hatua tano za ujenzi wa mabwawa, tumekamilisha hatua tatu ambazo ni upembuzi wa awali, upembuzi yakinifu na usanifu. Aidha, tumelipa jumla ya shilingi bilioni 7 kwa wananchi waliopisha ujenzi wa mradi huu. Serikali ipo katika hatua za mwisho za majadiliano na baadhi ya wadau wa maendeleo ili kupata fedha za kukamilisha ujenzi wa bwawa hili.
Kutokana na hatua mbalimbali zinazoendelea kuchukuliwa na serikali katika kupanua na kuimarisha miundombinu ya usambazaji katika Jiji la Dar es Salaama, hali ya upatikanaji wa maji imeboreka kutoka asilimia 55 mwaka 2015 hadi aslimia 75 mwezi Septemba 2017. Tunatarajia kuwa hali ya upatikanaji wa maji itaboreka zaidi na kufikia asilimia 86 ifikapo Juni 2018.

Usambazaji wa maji katika miji mikuu, miji midogo na halmashauri za wilaya
Serikali inatekeleza miradi mbalimbali katika ngazi ya miji mikuu ya mikoa na miji midogo 25. Miradi hii yote ina gharama ya zaidi ya shilingi trilioni 2.73 na ilipiwa na serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo. Baadhi ya miradi inayotekelezwa ni pamoja na mradi wa kuchukua maji kutoka Ziwa Viktoria na kupeleka katika miji ya Busega, Bariadi, Legangambili, Maswa, na Mwanhuzi, Isaka, Kagongwa, Mwadui, Kishapu, Kolandoto na Maganzo. Miradi yote kwa pamoja inagharimu jumla ya shilingi bilioni 763.
Mwezi Aprili mwaka huu, serikali ilisaini mikataba mitatu na wakandarasi watakaojenga mradi mkubwa wa maji unaotoa maji kutoka Ziwa Viktoria na kupeleka katika miji ya Tabora, Nzega, Uyui, Igunga, Tinde, na Sikonge. Mradi huu utagharimu jumla ya shilingi bilioni 600. Upo mradi mwingine unaotumia pia chanzo hiki cha Ziwa Victoria kwenda Miji ya Kagogwa na Isaka. Mradi huu unagharimu jumla ya Shilingi bilioni 24.72.
Miradi mingine imekamilika na/au inaendelea kutekelezwa katika miji mbalimbali ikiwemo: Mwanza, Bukoba, Musoma, Sengerema, Geita, Nansio, Kigoma, Sumbawanga, Lindi, Mtwara, Babati, Arusha, Morogoro, Mwanga, Same, Korogwe, Tanga, Mugumu, Longido, Simanjiro, Dodoma na Singida.
Aidha, serikali ipo mbioni kuanza kutekeleza mradi wa maji wa dola milioni 500 (zaidi ya shilingi trilioni 1) ikiwa ni mkopo nafuu kutoka serikali ya India kupitia Benki ya Exim-India. Mradi huu utatekelezwa katika miji 17, ikiwemo mji mmoja wa Zanzibar. Miji itakayofaidika na mradi kwa upande wa Tanzania Bara ni Muheza, Wanging’ombe, Makambako, Kayanga, Songea, Geita, Kilwamasoko, Tanga (HTM), Njombe, Mugumu, Chunya, Sikonge, Makonde, Manyoni, Kasulu and Rujewa.
Kwa hiyo, kwa ujumla wake, serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo imewekeza zaidi ya shilingi trilioni 3.73 katika miradi ya maji inayotekelezwa katika miji mikuu ya mikoa, miji mikuu ya wilaya na miji midogo. Kutokana na miradi inayoendelea kutekelezwa, tunatarajia hali ya upatikanaji wa maji kwa maeneo ya mijini iboreke kutoka chini ya asilimia 60 mwaka 2015 hadi asilimia 75 ifikapo Juni 2018 na kufikia wastani wa asilimia 95 ifikapo 2020.
Kwa upande wa Vijijini, Serikali kwa kushirikiana na Wadau wengine wa Maendeleo inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali kama sehemu ya Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP). Jumla  ya miradi 1,810 ilipangwa kutekelezwa maeneo ya vijijini tangu mwaka 2013, na kati ya hii, miradi 1,444 imekamilika, na miradi 366 ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji.
Katika kipindi cha miaka miwili ya utekelezaji wa awamu ya tano ya Serikali, jumla ya miradi 388 imeendelea kutekelezwa vijijini na kiasi cha shilingi 274,887,164,606.86 zimetumika kwa ajili ya miradi iliyokamilika na inayoendelea kutekelezwa.
Kwa ujumla, Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo, kupitia miradi mbalimbali iliyokamilika na inayoendelea, tayari imejenga vituo vya kuchotea maji vijijini 121,369, ukilinganisha na lengo la kujenga vituo 155,934 ifikapo mwaka 2020. Kama vituo hivi vyote vingefanya kazi vyote vingekuwa na uwezo wa kuwahudumia wananchi  milioni 30.3 sawa na asilimia 79. Hata hivyo, ni vituo 83,331 pekee vinavyofanya kazi vikiwa na uwezo wa kuhudumia watu milioni 20.8, sawa na asilimia 55. Hivyo, moja ya changamoto ya miradi ya maji vijijini ni kuhakikisha kuwa miradi inafanya kazi muda wote, na hili ni jukumu la Watumiaji pamoja na Uongozi katika ngazi ya Vijiji na Halmashauri. Serikali inachukua hatua mbalimbali kuimarisha usimamizi wa miradi iliyokamilika Vijijini. Lengo ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2020, angalau asilimia 85 ya wananchi vijijini wawe wanapata huduma ya maji.

Hitimisho
Katika miaka miwili ya uongozi wa Rais John Pombe Magufuli, serikali imeendelea kutekeleza na kuibua miradi mipya mbalimbali ya maji. Jumla ya miradi mikubwa mitano inatekelezwa Jijini Dar es Salaam, miradi zaidi ya 50 katika miji mbalimbali na miradi zaidi ya 1,800 vijijini.
Kukamilika kwa miradi inayoendelea kutekelezwa kutaongeza kasi ya usambazaji maji kwa wananchi. Lengo la serikali ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2020, angalau asilimia 85 ya wakaazi wa vijijini na asilimia 95 ya wakaazi wa mijini wawe wanapata maji safi, salama na ya uhakika. Kwa kushirikiana na wananchi na wadau wengine wa maendeleo, sisi watendaji katika serikali ya Rais Magufuli tunafanya kazi kwa bidii kubwa kuhakikisha kuwa lengo hili linatimia. Kasi ya utekelezaji wa miradi katika miaka miwili ya Rais Magufuli inaonesha pasi na shaka kuwa tutafikia malengo haya.
Mwandishi wa Makala haya ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

No comments:

Post a Comment