WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Friday, February 17, 2017

WASSIRA, BULAYA BADO NGOMA MBICHI

Wafuasi wa Steven Wassira Waendelea Kumng'ang'ania Ester Bulaya....


Wapigakura wanne wa Jimbo la Bunda waliofungua shauri kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliopita wameendelea kumng’ang’ania mbunge wa jimbo hilo, Ester Bulaya kwa kukata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu wa kutupa maombi yao.

Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Francis Kabwe alisema jana kuwa rufaa ya wapigakura hao, Magambo Masato, Matwiga Matwiga, Janes Ezekiel na Acetic Malagila iliyosajiliwa kwa namba 199 ya mwaka 2016, itasikilizwa mfululizo kuanzia Februari 20.

Alisema rufaa hiyo itasikilizwa jijini Mwanza na jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufani, Salim Mbarouk, Augustine Mwarija na Shabani Lila.

Katika maombi ya msingi waliyofungua Mahakama Kuu, wapigakura hao wanaowakilishwa na Wakili Constantine Mutalemwa, wanaiomba Mahakama kutengua ushindi wa Bulaya dhidi ya aliyekuwa mgombea wa CCM, Stephen Wasira kwa madai kuwa uchaguzi wa Oktoba 25, mwaka 2015 haukuwa huru na wa haki.

Pamoja na madai mengine, Masato na wenzake wanadai kuwa mchakato wa kampeni, upigaji kura na utangazaji wa matokeo uligubikwa na ukiukwaji wa sheria na utaratibu wa uchaguzi, vikiwamo vitendo vya rushwa, msimamizi wa uchaguzi kumnyima haki Wasira kwa kukataa ombi lake la kura kuhesabiwa upya.

Hoja nyingine ni msimamizi wa uchaguzi kutangaza matokeo bila Wasira kuwapo ukumbini na kuchanganya tarakimu za idadi ya wapigakura walioshiriki uchaguzi.

Novemba 17, mwaka jana, Jaji Noel Chocha wa Mahakama Kuu alimtangaza Bulaya kuwa mshindi halali wa uchaguzi huo baada ya kutupilia mbali maombi ya wapigakura hao.

No comments:

Post a Comment