WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Tuesday, October 18, 2016

BREAKING NEWS: MAFUTA NA GESI - ZITTO KABWE AWAPIGA TAFU WAZANZIBARI, AWASILISHA MUSWADA BUNGENI KUBADILI KATIBA

  ''Sheria Mpya ya 'Usimamizi, Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta Na Gesi Asilia' iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, ili kuanzisha kampuni ya maendeleo ya mafuta na gesi asilia Zanzibar ZPDC ambayo itashiriki katika shughuli za utafutaji na uendelazaji wa Mafuta na kesi asilia kwa niaba ya serikali ya Zanzibar''.

Zitto Kabwe  Mbunge wa Kigoma Mjini na Kiongozi wa ACT WAZALENDO

Taarifa ya Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini   (ACT-Wazalendo)
Ndugu Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto juu ya kuwasilisha Mswada wa Sheria ya Mabadiliko ya 15 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2016

Dodoma ,
Jumanne 18 Oktoba 2016,

Ndugu Wanahabari na Watanzania kwa Ujumla
Oktoba 8 mwaka huu, chama chetu cha ACT Wazalendo kilifanya Mkutano Mkuu wa Kidemokrasia (MMK) nchini, mkutano ambao ulifanyika katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa, jijini Dar es salaam. Lengo la mkutano husika lilikuwa ni kuwapa fursa Wanachama, Wafuasi, Wapenzi wa chama chetu, Wanaharakati, Wanahabari pamoja na Wananchi wa kawaida (ambao si wanachama wa ACT Wazalendo) ya kujadiliana kwa upana na Viongozi mbalimbali wa chama chetu juu ya masuala mbalimbali yahusuyo nchi yetu, ikiwa ni utaratibu mpya wa kisiasa nchini. 

Baada ya hotuba kutoka kwa viopngozi na wageni mbalimbali, pamoja na mijadala mipana kutoka kwa wanachama na wananchi mbalimbali, Mkutano Mkuu wa wa Kidemokrasia (MMK) ulitoa MAAZIMIO Kadhaa ya Kisera juu ya chama chetu na taifa kwa ujumla, maazimio ambayo ACT Wazalendo tuliahidi kuyabeba Na kuyapeleka kwenye Vikao vya Maamuzi ili yajadiliwe na kupitisho kuwa maamuzi rasmi ya chama. Mojawapo ya maazimio hayo ni suala la kuibua upya Mchakato wa Katiba Mpya nchini kwa kuanzia ilipoishia Tume ya Jaji Warioba. 

Suala jengine lililoibuka ni juu ya Sheria Mpya ya “Usimamizi, Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta Na Gesi Asilia” iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, ili kuanzisha kampuni ya maendeleo ya mafuta na gesi asilia Zanzibar ZPDC ambayo itashiriki katika shughuli za utafutaji na uendelazaji wa Mafuta na kesi asilia kwa niaba ya serikali ya Zanzibar. Sheria husika ilitungwa na kupitishwa mwezi huu na Baraza hilo la kutunga sheria Zanzibar katika vikao vyake vilivyomalizika karibuni. 

Mjadala mpana katika Mkutano wetu Mkuu wa Kidemokrasia (MMK) ulionyesha kwa dhahiri kuwa pamoja na Baraza la Wawakilishi la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kutunga Sheria hiyo, bado Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) haipati “Uhalali wa Kisheria na Kikatiba” juu ya usimamizi, utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia kwa upande wa Zanzibar.

Wanasheria mbalimbali walieleza kuwa vikwazo vya Kisheria na Kikatiba vitawafanya hata Wawekezaji wa sekta ya mafuta na gesi asilia kutothubutu kufanya uwekezaji Zanzibar, na hivyo kuwanyima fursa Wazanzibari ya kufaidika na rasilimali za Taifa letu. 

Sekretarieti ya chama cha ACT Wazalendo ilikaa na kufanya9 uchambuzi juu ya masuala yote ya Kisera ambayo yaliibuliwa katika Mkutano Mkuu wa Kidemokrasia (MMK). Na Miongoni mwa mambo ambayo chama chetu kupitia vikao vyake halali kimeamua kuyabeba ni hilo la “Sheria ya Usimamizi, Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia”, ambayo baada ya mjadala mpana wa Kisheria ilionekana ni dhahiri kuwa Sheria husika ni batili kwakuwa inakwenda kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977. 

Kamati ya Katiba na Sheria ya Chama cha ACT Wazalendo kupitia mimi Mbunge wake imeonelea ni vema kuwasilisha Bungeni “Mswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Kumi na Tano (15) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 2016” (juu ya masuala ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar). Lengo la mabadiliko hayo likiwa ni “Kuiwezesha Zanzibar Kupata Uhalali wa Kisheria na Kiakatiba juu ya Uendelazwaji wa Sekta ya Mafuta Na Gesi Asilia”. 

Na hivyo kuondoa vikwazo vya Kikatiba na Kisheria vilivyoko sasa ambapo mamalaka hayo ya Usimamizi, Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia bado Kisheria na Kikatiba yako chini ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hata mara baada ya kupitishwa kwa Sheria hii ya Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. 
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein.

Pamoja na kwamba ACT Wazalendo tumeamua kupigania kuufufua upya Mchakato wa Katiba Mpya lakini bado tumeonelea umuhimu mkubwa wa kuleta Bungeni mabadiliko haya ya 15 ya Katiba tuliyonayo sasa, mabadiliko ambayo yatanusuru uvunjwaji wa Katiba tuliyonayo sasa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kusubiri Katiba Mpya hakuhalalishi Katiba ya Mwaka 1977 tuliyonayo sasa kuvunjwa. Kwa kuwa mchakato wa mabadiliko ya Katiba Mpya umekwama bila Kauli ya Serikali wala Muafaka wa Kitaifa juu ya lini mchakato huo utaendelea, "Muswada huu Binafsi" ni hoja ya lazima kwa sasa katika kuhalalisha hatua ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) ya kutunga sheria juu ya Usimamizi, Utafutaji na  Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia kwa Upande wa Zanzibar

Ni imani yangu, pamoja na changu kuwa Bunge litaona busara iliyoko mbele ya Mswada huu, na kwa Uharaka itaona umuhimu wa kuruhusu mjadala wake Bungeni ili kutoifanya Sheria hii ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar kuwa kero Mpya ya Muungano wetu. 

Naamini, nitaweza kushirikiana na Wabunge wenzangu Bungeni, pindi mswada huu utakapopangiwa tarehe ya kuletwa kwaajili ya mjadala, kuhakikisha tunatimiza wajibu wetu wa kizalendo wa kuhakikisha Watanzania Wote, kutoka pande zote mbili za Muungano, wanafaidika na Rasilimali za Taifa letu. 

Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.

No comments:

Post a Comment