WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Thursday, October 13, 2016

ORODHA KAMILI YA WASALITI WA KISIASA HII HAPA


Maalim Seif Sharrif Hamad .
'' Maalim Seif naye aliitwa msaliti wa Wazanzibari kwa madai kuwa mwaka 1984 ndiye aliyepika maneno kwenda kwa Mwalimu Nyerere dhidi ya Rais wa Pili wa Zanzibar, Aboud Jumbe Mwinyi. Kwamba ni maneno hayo yaliyosababisha Jumbe aondolewe urais wa Zanzibar na kunyang’anywa vyeo vyote alivyokuwa navyo kwenye chama cha CCM na Serikali.''

Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alimuita rafiki yake wa harakati za kisiasa aliyegeuka hasimu wake, Oscar Kambona kuwa msaliti akisema kuwa alitumiwa na Wazungu kufitini Serikali ya Tanganyika na baadaye Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kambona naye kwa maelezo yake ni kwamba Mwalimu Nyerere alimsaliti kwa sababu walishirikiana kudai uhuru wa nchi baada ya kuwa rais, alimfanya aishi kama mkimbizi nchini Uingereza.
Usaliti katika siasa ni jicho la mtu. Kama mlikuwa pamoja kisha mkatofautiana, neno msaliti lazima lipewe nafasi.

http://www.bongocelebrity.com/wp-content/uploads/2011/04/Oscar_Kambona-1.jpg 
Oscar Kambona.

Mwalimu Nyerere alimuita Bibi Titi Mohamed ni msaliti, vilevile mwanamke huyo wa shoka alidai kusalitiwa na Mwalimu Nyerere.
Usaliti kwenye kamusi ya kisiasa ni kutofautiana. Mnapokuwa kwenye chama kimoja cha siasa kisha mkawa hamuendani na mambo fulani fulani, lazima atokee mtu wa kumuita mwenzake msaliti.
Wanasiasa hulitamka neno msaliti wakijua kabisa ni baya. Usaliti kwa maana yake ni kitendo cha kwenda kinyume na makubaliano.

Tafsiri hiyo haipo kwenye kamusi ya wanasiasa. Wao ndani ya chama kimoja wanapotofautiana mitazamo huo huitwa usaliti. Anayeanza kumtamka mwenzake mara nyingi ndiye hufanikiwa.
 http://www.awaazmagazine.com/previous/media/k2/items/cache/617a2776f20d4e817afffbdbb257cffa_XL.jpgBibi Titi Mohamed katika moja ya matukio ya kihistoria.

Neno usaliti linavunja heshima, linachafua, kwa hiyo ukishaitwa hivyo, unakuwa kama vile umemwagiwa takataka ngumu, popote unapopita watu watanyoosheana vidole kuwa wewe ni msaliti.

Usaliti ni ‘ukutiukuti’

Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad alimsema aliyekuwa Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni katika Bunge la Tisa, Hamad Rashid Mohamed kuwa ni msaliti aliyehongwa fedha ili awagawe Wazanzibari katika kudai haki zao ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Maalim Seif naye aliitwa msaliti wa Wazanzibari kwa madai kuwa mwaka 1984 ndiye aliyepika maneno kwenda kwa Mwalimu Nyerere dhidi ya Rais wa Pili wa Zanzibar, Aboud Jumbe Mwinyi. Kwamba ni maneno hayo yaliyosababisha Jumbe aondolewe urais wa Zanzibar na kunyang’anywa vyeo vyote alivyokuwa navyo kwenye chama cha CCM na Serikali.

Hata sasa, Maalim Seif anamuita Profesa Ibrahim Lipumba msaliti ni kama ambavyo Lipumba naye alivyosimama kidete kumshughulikia Hamad Rashid kwa hoja ya usaliti. Kimsingi usaliti kwenye siasa ni kama mchezo wa watoto kuzunguka kwa mduara ambao unaitwa ukutiukuti.

Seif aliitwa msaliti wa Wazanzibari kipindi cha Jumbe, naye sasa anawaita Rashid na Lipumba jina hilo. Akina Lipumba pia hoja yao ni kwamba Maalim Seif ni msaliti. Ni kutuhumiana na kuchafuana.
Mgogoro wa Rashid CUF ulitokana na dhamira yake ya kuwania Ukatibu Mkuu, cheo ambacho kipo kwenye mikono ya Maalim Seif. Rashid katika kutetea dhamira yake alisema kuwa Maalim Seif baada ya kupata Umakamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar alikidhoofisha chama.

Rashid alitaka Maalim Seif aache Ukatibu Mkuu wa CUF ili yeye ashike nafasi hiyo apate kukijenga chama. Ni hapo ndipo usaliti wa Rashid ulisemwa kila upande. Kashfa mbaya zaidi aliitwa msaliti wa Wazanzibari.
Ipo hoja inayozungumzwa dhidi ya Maalim Seif. Vinazungumzwa vipindi ambavyo moto uliwaka kati ya CUF na polisi, haipo mara moja ambayo Maalim Seif alisimama mstari wa mbele, mara zote haonekani.

Upande wa Lipumba hivi sasa wanasema kuwa zipo picha zinazomuonyesha akiwa chini ya ulinzi wa polisi na zile ambazo amepigwa na kuumizwa. Wanahoji zilipo picha Maalim Seif akiwa CUF zenye kumuonyesha akipambana na polisi, kukamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi au za kupigwa japo mara moja.
Machafuko makubwa ya kisiasa kuwahi kutokea nchini ya Januari 26 na 27, 2001, Zanzibar na Dar es Salaam, wanasema Lipumba alipigwa, kuvunjwa mkono na kuwekwa mahabusu pamoja na wafuasi wengine wengi wa CUF. Wanahoji Seif alikuwa wapi? Hitimisho lao ni kuwa Seif ndiye msaliti.

Kikwete na Lowassa

Kauli ya Waziri Mkuu wa zamani, aliyetumika katika Serikali ya Awamu ya Nne, Edward Lowassa ni kuwa Rais mstaafu, Jakaya Kikwete alimsaliti kwa sababu walikubaliana kushirikiana kisha kuachiana uongozi.
Siri hii iliyotoka kwa Lowassa ni kuwa katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2005, hakuchukua fomu ya kugombea urais kwa sababu alimuunga mkono JK na makubaliano yakawa baada ya JK kumaliza muda wake, alipaswa kumsaidia Lowassa.
 http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/3052200/medRes/1156879/-/mya968/-/Lowassa.jpg
 Edward Lowassa Mjumbe wa Kamati kuu CHADEMA.

Vilevile, Lowassa naye anaitwa msaliti, aliyejaribu kumzunguka JK alipokuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM. Zipo fitina ambazo Lowassa anatuhumiwa kuzitengeneza ili kumdhoofisha JK.

Katika siasa unapomuona mtu anaitwa msaliti, usikimbilie kumhukumu, maana ukimuuliza naye atakutajia wasaliti wake. Anayeita wenzake wasaliti, ukifuatilia upande wa pili naye jina hilo linakuwa linamhusu.
Usaliti kwenye siasa ni vita ya masilahi. Ukionekana unaingilia masilahi yake lazima akuite msaliti. Katika siasa kama mtatofautiana bila kuathiri masilahi ya kila upande ni vigumu neno usaliti kusikika.
 http://mwanahalisionline.com/wp-content/uploads/2015/07/Lowassa-na-Kikwete-620x310.jpgwaheshimiwa Edward Lowassa na Jakaya Kikwete wakiwa jukwaani.

Popote utakaposikia mwanasiasa ameitwa msaliti, ujue kuna masilahi ya watu kaingilia. Na ukisikia mwanasiasa anamuita mwenzake msaliti, tambua masilahi yake yameguswa.
Profesa Abdallah Safari alitofautiana na Lipumba CUF, lakini hakuitwa msaliti kwa sababu hakuonekana kugusa masilahi ya Lipumba. Safari hakuwa na madhara kwa uenyekiti wa Lipumba.

Rashid aligusa masilahi ya watu alipotaka kushika nafasi ya katibu mkuu ndiyo maana vita ilikuwa kubwa.

Usaliti Chadema

Kote wanaweza kuitana wasaliti, lakini Chadema wamenyoosheana zaidi vidole. Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Tanzania Bara ambaye sasa ni Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ana rekodi pana ya kuitwa jina hilo.
 https://zittokabwe.files.wordpress.com/2011/02/katibu_mkuu_wa_chadema_dr__wilbroud_slaa_akisalimiana_na_naibu_kiongozi_wa_kambi_ya_upinzani_bungeni_zitto_kabwe_leo_.jpg
Dkt. Slaa akiwa na Zitto Kabwe.
Zitto aliitwa msaliti kwa sababu ya kutofautiana na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na aliyekuwa Katibu Mkuu, Dk Willibrod Slaa. Hoja kuu iliyojengwa ni kuwa Zitto alikuwa anapokea fedha nyingi kutoka CCM na Serikali yake na kuzitumia kukivuruga chama.

Kabla ya Zitto, aliyeitwa msaliti ni aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, Chacha Wangwe baada ya mzunguko huo, Dk Slaa naye akawa msaliti kuanzia mwaka jana mpaka sasa.

Usaliti hata Urusi

Usaliti ni vita ya masilahi; Katika Chama cha Ujamaa wa Kidemokrasia cha Urusi na baadaye Chama cha Kikomunisti, kulikuwa na vijana wanne wenye maono na itikadi za kikomunisti ambao ni Leon Trotsky, Joseph Stalin, Grigory Zinoviev na Lev Kamenev. Hapo ni kuanzia mwishoni mwa Karne ya 19 mpaka katikati ya Karne ya 20.

Mwaka 1917, Urusi na Dola ya Umoja wa Nchi za Kisovieti vikiwa chini ya uongozi wa nembo ya ukomunisti, Vladimir Lenin, vijana hao wanne waliingizwa kwenye chombo kikuu cha uamuzi katika chama na Serikali (Politburo) kama sehemu ya wajumbe saba waanzilishi.

Trotsky alimuunga mkono Lenin waziwazi na alionekana ni kijana mwenye akili nyingi maana baadhi ya dhana zake za kiuongozi zilitumiwa pia na kiongozi huyo. Watu wengi Urusi wakati huo, waliamini mwisho wa Trotsky ungekuwa kuongoza Dola ya Kisovieti.

Stalin hakumpenda Trotsky na alimuona ni mtu hatari kwa masilahi yake ya kisiasa, kwa hiyo akawashawishi Zinoviev na Kamenev, wakaunda utatu wa kisiasa na kidola ambao waliuita Triumvirate, wakijilinganisha na utatu wa Julius Caesar, Pompey na Crassus waliounganisha nguvu ili kuitawala Roma miaka 60 Kabla ya Kristo.

Trotsky akajikuta kwenye mapambano na Triumvirate. Stalin hakuwa na ushawishi mkubwa, hivyo aliwatumia Zinoviev na Kamenev kumshughulikia Trotsky kwenye chama na serikalini. Trotsky akaitwa msaliti jina likakua.

Baada ya Trotsky kupungua nguvu, Stalin aliwageuka Zinoviev na Kamenev akawachachafya kuwa nao ni wasaliti. Alifanikiwa maana Aprili 3, 1922, Stalin alikamata mamlaka ya chama na Dola ya Kisovieti.
Hata baada ya kukamata nafasi hiyo, Stalin alimhofia Trotsky, hivyo ili kuzidi kumchafua alihakikisha anatambulika rasmi serikalini kama msaliti kwa jina la Yuda Trotsky, yaani Msaliti Trotsky. Oktoba 23, 1926, Stalin alitumia mamlaka yake kushawishi na kumfukuza Trotsky kwenye chama na kumuondoa kwenye vyeo vyote.

Mwaka 1940, Trotsky aliuawa na ikaaminika kuwa Stalin alihusika na mpango huo wa mauaji. Upande mwingine, Zinoviev na Kamenev walimuona Stalin ni msaliti na mtu hatari, maana walishirikiana kwa utatu wao kumshughulikia Trotsky baada ya kufanikiwa aliwageuka.

Mwandishi wa makala haya ni Luqman Maloto, mwandishi wa habari, mchambuzi wa siasa, jamii na sanaa.
Ni mmiliki wa tovuti ya Maandishi Genius inayopatikana kwa anuani ya mtandao

No comments:

Post a Comment