WADHAMINI WETU

WADHAMINI WETU

Sunday, October 16, 2016

SAKATA ESCROW BADO BICHI : KADA CHADEMA AMVAA RAIS MAGUFULI.

''Mhe rais, chukuwa hatua. Sitisha fedha za malipo hayo haramu tuonawalipa PAP kila mwezi. Fumua shirika letu la umeme kwa kuondoa matapeli wote hasa wale ambao wapo kwenye eneo la sheria. Hawa wana undugu wa damu na matapeli''.
 Harbinder Singh Sethi kushoto na Joseph Makandege Kulia.
 
MHE RAIS, KATIKA HILI LA IPTL, BORA LAWAMA KULIKO FEDHEHA!
------------------------------

Mhe Rais, pole na majukumu mazito ya kuiongoza nchi katika mazingira magumu. Natambua pia kazi kubwa uliyonayo hasa ya utekelezaji wa ahadi zako kwa wananchi hasa ile ya kulinda fedha za umma.
Mhe Rais, nchi yetu kwasasa inapitia wakati mgumu hasa wa kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Inasikitisha kwamba, bado nchi hii inakabiliwa na upungufu mkubwa wa dawa  mahospitalini na wanafunzi wengi ambao uliwaahidi kuwa wangepata mikopo kwajili ya elimu zao za juu, wengi wao wamekosa mikopo hiyo.

Mhe rais, lengo langu sio kuainisha ugumu ambao tunapitia kama taifa, kwasababu nikifanya hivyo, huenda andiko hili likawa refu sana au kuitwa la kichochezi. Muhimu nimelenga kukuonesha au kukumbusha, eneo ambalo linakutia doa sana au kukupa sifa mbaya katika vita ya kupambana na vitendo vya rushwa, ufisadi na aina zote za uhujumu uchumi wa nchi yetu. Matarajio ya wengi ni kukuona ukiwa na 'ZERO TOLERANCE' kwenye eneo hili.

Swala la IPTL ni tatizo kubwa kwa nchi yetu kwasababu sio tu kwamba linatutia hasara kama nchi, bali linakufedhehesha kama kiongozi wa nchi.

Wengi wetu tumeshindwa kuelewa hasa ni kipi ambacho kimepelekea matapeli hawa kuendelea kuturudisha nyuma kama taifa na wakati tunaye rais ambaye anaonekana kujipambanua kushughulika na wezi, wahujumu uchumi na wala rushwa?

Tunajiuliza, hivi kiongozi wetu wa nchi ambaye ameonesha nia ya kubana matumizi ya serikali na kupunguza anasa katika utumishi wa umma, anaweza vipi kushuhudia utapeli wa mchana kweupe uliofanywa na unaoendelea kufanywa na matapeli wa ndani na wa nje bila kuchukuwa hatua yoyote? Binafsi siamini kama umeshindwa kuchukuwa hatua dhidi ya matapeli hawa.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombr Magufuli.

Mhe Rais, hukumu ya ICSID inatutaka tuwalipe SCB HK ambao ndio wamiliki halali wa IPTL kiasi cha shilingi bilioni 320($148m). 

Mwaka 2013 tuliwalipa PAP(matapeli) zaidi ya bilioni 300. Hii ni baada ya matapeli hao na ndugu zao kutoka shirika letu la umeme kwa baraka za baadhi ya viongozi wa serikali kukutana pale Kunduchi Beach Hotel & Resort October 3, 2013 kuanzia saa 17:00-02:38 kwajili ya kupanga namna ya kutupiga bila sisi kujua. 

Kikao hicho kilichokuwa na wajumbe 6 na ajenda 6, pamoja na mambo mengine, kilifanikiwa kubadilisha hukumu halali kwa kuamua fedha za kwenye A/C ya Tageta Escrow pamoja na mitambo ya uzalishaji umeme, vyote vikabidhiwe kwa PAP. 

Mhe rais, pamoja na BOT kuiandikia wizara ya nishati na madini barua ya kutowaruhusu PAP kutoa fedha kwenye A/C(Nov 28 & 05 Dec 2014),matapeli hao walifanikiwa kutoa fedha hizo na kuanza kugawana kama peremende.

Mhe rais, matapeli hao hasa wale ambao wako kwenye shirika letu hodhi na wale wa wizara husika licha ya kwamba mpaka leo wapo salama kabisa, watu hao na wengineo ambao ni ndugu wa damu na tabia, wamezoea kutubia. 
Ni hisia zangu kwamba swala kwamba tunaibiwa huwenda unalifahamu.
Utakuwa na kumbukumbu kwamba 2012  tuliwalipa isivyo rasmi Dowans zaidi ya bilioni 140 ambazo hadi leo hazipo kwenye vitabu vya bajeti.

Hata tukiwalipa SCB HK hizo dola 148m hiyo haitakuwa mwisho wa kuibiwa na matapeli hao kwakuwa tayari tunalo deni la kulipa katika siku za usoni ambalo chimbuko lake ni utapeli uliofanyika dhidi ya kampuni ya Symbion  kwa sisi kuvunja mkataba nao wa miaka 15 baada ya kugundua ulikuwa wa kitapeli. Business as usual!

Mhe rais, licha ya serikali yako kukosa bilioni 42.5 sawa na 68% za kuipa MSD kwajili ya dawa hospitalini mwezi July mpaka September, kila mwezi tunawalipa IPTL zaidi ya bilioni 7 kila mwezi kwajili ya mitambo inayotokana na mkataba huo wakitapeli. Inauma sana kwasababu hatupaswi kuwalipa fedha zinazotokana na kitu haramu.

Mhe rais, chukuwa hatua. Sitisha fedha za malipo hayo haramu tuonawalipa PAP kila mwezi. Fumua shirika letu la umeme kwa kuondoa matapeli wote hasa wale ambao wapo kwenye eneo la sheria. Hawa wana undugu wa damu na matapeli. Hawa wanatuhujumu. 

Hawana tofauti na vibaka wa Kariakoo wanaojifanya wanamfukuza mwizi kumbe ni ndugu yao. Bila kufanya hivyo, hatua yoyote utakayochukuwa, Matapeli hao kwa kujua ndugu zao ndio wako kwenye safu ya ulinzi, watakimbilia mahakamani na watatushinda vizuri tu. 

Mhe rais, kwasababu chimbuko la utapeli mwingi hutokana na upungufu wa nishati ya umeme, ruhusu mashirika na makampuni binafsi kuzalisha nishati hiyo. Hii itaongeza ufanisi utakaotokana na ushindani baina yao. 

Wananchi tunahitaji Nishati ya umeme sio nishati ya umeme inayotokana na  la shirika la umma. Tunahitaji iwe kama kwenye huduma za usafiri wa anga ambapo ATCL inashindana na mashirika binafsi.
Mhe rais, washughulikie wote ambao wametuumiza na wanaoendelea kutuumiza. 

Kwa kufanya hivyo, utakuwa umeweka precedent sahihi na hisia kwamba unawalinda mafisadi na matapeli Hawa hazitakuwepo. Najua wapo wakubwa, washughulikie tu  utakumbukwa kwa hilo na hapa ndipo nia yako ya kupambana na ufisadi itakapodhihirika kwa usahihi wake. 

Bora lawama kuliko fedheha!
Matarajio ya watanzania ni kusikia kishindo kizito katika siku za hivi karibuni cheenye baraka zako au ukimya wenye baraka zote kutoka kwako.
Mungu ibariki Tanzania.

 IMEANDIKWA 
Na. Bob Chacha Wangwe
October 16, 2016

No comments:

Post a Comment